• Nairobi
  • Last Updated May 12th, 2024 5:17 PM
Jinsi ya kuandaa shawarma ya minofu ya kuku

Jinsi ya kuandaa shawarma ya minofu ya kuku

Na MARY WANGARI

KATIKA jiko letu leo, tutajifunza jinsi ya kuandaa mlo mtamu wa shawarma ya minofu ya kuku.

Kwanza kabisa, shawarma ni chakula chenye asili yake Uarabuni.

Chakula hiki ni rahisi kuandaa na mwafaka kula wakati wowote maadamu ni chepesi na kinachosheheni viinimwili muhimu kiafya hata pasipo kula sana.

Viungo unavyohitaji

1 kilo kuku

½ lita mafuta ya kupikia. Napendelea kutumia mafuta ya zeituni (Olive oil) lakini unaweza kutumia uyapendayo.

1 kijiko kikubwa cha chumvi

1 kijiko kidogo cha pilipili manga

2 pilipili hoho kubwa

2 vitunguu maji vikubwa

1 kikubwa cha kitunguu saumu kilichosagwa

3 karoti kubwa

1 ndimu au limau. Ukipenda unaweza pia kutumia siki (vinegar)

2 vijiko vya curry powder

3 tortilla au ukipenda chapati zilizopikiwa kwenye oven.

Maandalizi ya Tortilla au chapatti

Kwenye karai safi weka unga wa ngano, sukari, chumvi na hamira koroga hadi vichanganyike vyema.

Mimia maji au maziwa vuguvugu kanda unga wako hadi ushikamane vyema, si mwepesi si mgumu kisha weka pembeni uumuke.

Kata madonge kisha sukuma kama unavyofanya chapati za kawaida.

Kwenye kikaangio, choma chapatti zako bila mafuta kisha uziweke kando zipoe.

Maandalizi ya kuku

Osha kuku wako na kisha umkatekate vipande vidogovidogo ili viweze kuiva vizuri na upesi.

Katika karai safi tia vipande vya kuku, kamulia limau, nyunyizia chumvi, kitunguu saumu, na tangawizi huku uikendelea kuchanganya ili viungo vikolee vyema.

Weka nyama yako pembeni kwa muda wa saa moja.

Safisha viungo vilivyosalia: kitunguu maji, pilipili mboga na karoti.

Menya karoti na kitunguu maji kisha uvikate vipande vidogovidogo.

Kisha pilipili hoho ikate vipande virefu na vipana. Vitapendeza zaidi kwenye msosi wako.

Chukua kikaangio chako ukibandike kwenye moto na umiminie mafuta.

Yakisha pata moto tia nyama uliyounga hapo awali na uitandaze vizuri.

Subiri iive kwa dakika 10 kisha igeuze ili iive vizuri upande wa pili.

Endelea kugeuza mara kwa mara ili iive vizuri na kukauka maji.

Ikianza kubadilika rangi ongeza pilipili manga na ukoroge vizuri.

Baada ya dakika tano epua nyama na uiweke pembeni katika sinia safi.

Bandika kikaangio safi motoni weka mafuta na yakisha pata moto weka kitunguu maji.

Kaanga kitunguu na kikianza kubadilika rangi ongeza pilipili hoho, karoti, na ukoroge vyema.

Subiri baada ya dakika 5 ongeza nyama ya kuku na uchanganye vyema.

Ongeza curry powder na ukoroge vyema hadi iingiane vyema kwenye mchanganyiko huo.

Epua na uweke pembeni.

Chukua chapati ulizoandaa awali, paka sauceau mayonnaise uipendayo, kisha weka salad kisha nyama, mwagia sauce juu kisha izungushe na uchome na vichokoneo (tooth pick) ili isifunguke.

Msosi wako upo tayari kwa kuliwa. Jiburudishe.

You can share this post!

DOMO KAYA: Asante ya punda mateke

Timu kubwa Kenya zaumia kutokana na ukosefu wa viwanja