NA WANDERI KAMAU
USIMAMIZI wa mikakati ya kuboresha zao la kahawa katika ukanda wa Mlima Kenya umegeuka kuwa chanzo cha makabiliano makali baina ya Naibu Rais Rigathi Gachagua na Waziri wa Kilimo Mithika Linturi.
Ni juhudi ambazo pia zinatishia kufufua upya tofauti za kisiasa baina ya ukanda wa Mlima Kenya Mashariki na Magharibi.
Kufuatia mpangilio mpya wa serikali uliotolewa na Rais William Ruto wiki iliyopita, baadhi ya viongozi katika eneo la Mlima Kenya Mashariki wamelalamikia “kupunguzwa” kwa mamlaka ya Bw Linturi na kukabidhiwa Bw Gachagua, anayetoka Mlima Kenya Magharibi.
Mlima Kenya Magharibi inazishirikisha kaunti za eneo la Kati, zikiwemo Nyeri, Nyandarua, Murang’a, Kirinyaga na Kiambu.
Ukanda wa Mashariki unazishirikisha kaunti za Meru, Embu na Tharaka Nithi.
Kwenye mpangilio huo, Rais Ruto alimtengea Bw Gachagua jukumu la kusimamia na kuendesha mikakati ya kuleta mageuzi katika sekta za kahawa, majanichai, ufugaji kati ya mazao mengi.
Hata hivyo, Bw Gachagua amekuwa akionekana kupigia debe mageuzi katika sekta ya kahawa, ikizingatiwa inakuzwa kwa wingi katika eneo hilo.
Viongozi kadhaa kutoka Mlima Kenya Mashariki wamejitokeza kulalamikia mpangilio huo, wakiutaja kuwa “mwendelezo wa juhudi za kulitenga eneo hilo kisiasa na kuliweka chini ya Magharibi”.
“Mpangilio huu ni juhudi za makusudi kufufua upya ubabe wa kisiasa ambao umekuwepo baina ya jamii ya Agikuyu kwa upande mmoja, na jamii za Wameru, Watharaka na Waembu kwa upande mwingine,” akasema mbunge mmoja kutoka Kaunti ya Meru, ambaye hakutaka kutajwa.
Kulingana naye, ingekuwa vizuri ikiwa Rais Ruto angemwachia Bw Linturi jukumu hilo, kwani lipo chini ya Wizara ya Kilimo.
“Ijapokuwa Rais Ruto ana nia safi kwenye mpangilio huo mpya, ni hatua itakayozua uhasama, migongano na mivutano isiyofaa ya kisiasa baina ya viongozi hao wawili. Matokeo yake yatakuwa ufufuzi wa uhasama wa jadi wa kisiasa ambao umekuwepo baina ya jamii za GEMA,” akaeleza Bw Kipkorir Mutai, ambaye ni mchanganuzi wa siasa.
Viongozi kutoka Mashariki waliozungumza na ‘Jamvi la Siasa’ walisema kwamba kwa kumpa Bw Gachagua jukumu la kuongoza harakati za kufufua sekta ya kahawa, Rais Ruto ameonekana kupuuza changamoto zinazokumba uzalishaji wa mazao mengine kama vile miraa.
Walisema kuwa waliwashinikiza wakazi katika eneo hilo kuichagua serikali ya Kenya Kwanza kwa ahadi ya kufufua kilimo cha zao la miraa, ambacho mapato yake yamedorora kwa miaka kadhaa iliyopita.
Wadadisi wanasema malalamishi hayo mapya yanafaa kumfungua macho Rais Ruto, kwani huenda yakampotezea uungwaji mkono katika moja ya ngome zake kuu za kisiasa ielekeapo 2027.
“Ingawa Rais Ruto ameonyesha juhudi za kulirudishia mkono eneo la Mlima Kenya kwa kumpigia kura kwa wingi kwenye uchaguzi wa Agosti 9, 2022,” alisema.
Subscribe our newsletter to stay updated