KWA HISANI YA KENYA YEARBOOK
SULEIMAN Rashid Shakombo hakuwa akifahamika kabisa eneo la Likoni kabla ya kujiunga na siasa mwaka wa 1997.
Aliacha utawala wa mikoa na akiungwa na chama ambacho hakikuwa maarufu, alimshinda Khalif Salim Mwavumo aliyekuwa wa chama kilichokuwa maarufu cha Forum for the Restoration of Democracy-Kenya (FORD-Kenya) ambacho miaka mitano iliyotangulia 1992, alikuwa amemshinda mgombeaji wa chama kilichokuwa vigumu kushinda tangu uhuru cha Kenya African National Union (KANU).
Shakombo alikuwa wa kwanza na wa pekee nchini kutoka chama ambacho hakikuwa kimesikika cha Shirikisho Party of Kenya (SPK) kuwahi kushinda kiti cha ubunge.
Aliibuka kuwa shupavu katika siasa za eneo lake la nyumbani na siasa za kitaifa, wachanganuzi walifikiria kwamba alikuwa mwepesi wa kutambua mambo. Shakombo alithibitisha haya punde tu baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2002, alipohamia chama tawala cha KANU bila kuarifu SPK, miezi michache kabla ya tarehe ya uchaguzi, na kusababisha mzozo ndani ya chama hicho.
Suala hili lilifikishwa katika meza ya Jaji Mkuu Bernard Chunga atoe mwelekeo kuhusu iwapo korti ya Kikatiba ilipaswa kutatua fumbo ambalo lilipokonya chama hicho sauti yake ya pekee Bungeni.
Lakini Jaji Mkuu ambaye enzi hizo alikuwa ameteuliwa na Rais alikuwa kwenye kizungumkuti pia- kwa kuwa Shakambo alikuwa ametangaza kuhama kwake akiwa Ikulu ambapo alikuwa amealikwa na Rais Daniel arap Moi na alipokewa katika KANU na Kiongozi wa nchi mwenyewe.
Kesi kama hizo zilikuwa zimegonga mwamba na Chunga hangeweza kufanya chochote. Mikono yake, inavyosemwa, ilikuwa imefungwa. Bila chaguo, SPK ilijaza nafasi ya Shakombo kama mwenyekiti na Mashengu wa Mwachofi.
Chama kilitumainia kwamba uchaguzi uliokuwa karibu ungekifanya kupata Wabunge wengine lakini hakuna mbunge mwingine alitoka katika chama hicho zaidi ya muongo mmoja.
Hesabu ya KANU haikukisaidia; chama hicho hakikujua kilikuwa kikijihusisha na nani. Uchaguzi ulipofika, Shakombo alibadilisha nia, na akahamia muungano ulioongozwa na Kibaki wa National Rainbow Coalition, NARC, ambao ulikuwa umepigiwa upatu kusababisha Tsunami kote nchini na kuwa wazi ungetwaa mamlaka kutoka kwa KANU.
Shakombo alikuwa akielewa na kujua utamu wa madaraka kutoka enzi zake katika Utawala wa Mikoa ambako alipanda cheo kuwa Mkuu wa Wilaya na Naibu Katibu.
Alikuwa akitaka mamlaka alipohamia KANU lakini akabaini kuwa nguvu za chama hicho katika Ikulu zilikuwa zikilegezwa na tsumani ya NARC.
Alikuwa mjanja wa kusoma joto la kisiasa na mnamo Desemba 27 alihifadhi kiti chake kwa urahisi kwa tikiti ya chama hicho.
Hakuwa mtu wa kupumzika. Shakombo alitia bidii kumvutia Rais akitumia kila fursa ikiwemo kufika katika uwanja wa ndege na kujitokeza katika ziara zote za Kibaki alipozuru Pwani.
Aliendelea kucheza karata yake akilenga kutimiza ndoto zake. Pengine hakuna kinachoelezea hulka hii vyema kama uamuzi wake kufuatia kifo cha Karisa Maitha mwaka wa 2004.
Aliungana na mbunge wa Changamwe Ramathan Seif Kajembe kulalamika wakati Mahakama ya Mombasa ilijaribu kusimamisha uteuzi wa Ali Hassan Joho na NARC kugombea kiti cha ubunge cha Kisauni.
Shakombo alisubiri kwa uvumilivu kwa miaka mitatu kabla ya ndoto yake kutimia. Kuelekea mwisho wa 2005, aliteuliwa Waziri wa Urithi wa Taifa na Utamaduni katika Afisi ya Rais. Shakombo aliheshimiwa na kuaminiwa na wenzake katika eneo la Pwani ambao Februari 2003, walimchagua mwenyekiti wa Kundi la Wabunge wa Pwani kuomba serikali kufufua viwanda vilivyoporomoka eneo hilo.
Shakombo alikuwa miongoni mwa washirika wa karibu wa Kibaki waliopoteza viti vyao katika uchaguzi mkuu wa 2007.
Baada ya miaka miwili kwenye baridi, Kibaki alimteua mwenyekiti wa kampuni ya Kenya Petroleum Refineries Limited mwaka wa 2009, wadhifa ambao aliteuliwa tena kuushikilia na Rais Uhuru Kenyatta mwaka wa 2015.
Subscribe our newsletter to stay updated