• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
Kwake, fursa ya kumsalimia Mzee Jomo Kenyatta ilikuwa ni ya kipekee

Kwake, fursa ya kumsalimia Mzee Jomo Kenyatta ilikuwa ni ya kipekee

Na SAMMY WAWERU

MZEE Jomo Kenyatta alikuwa kiongozi aliyethamini bidii katika kazi.

Kulingana na Moses Gitonga, ambaye amewahi kuhudumu katika kikosi cha jeshi la Kenya, chini ya utawala wa Rais huyo mwanzilishi wa taifa hili, aliyepata fursa kutangamana naye lazima angekuwa mhudumu mchapakazi.

Gitonga alihudumu katika kikosi cha jeshi kwa muda wa miaka mitano pekee.

Ni mwalimu kitaaluma, ila aliacha gange hiyo kujiunga na jeshi la Kenya.

“Nilikamilisha kozi ya mafunzo ya ualimu mwaka wa 1974, nikafunza mwaka mmoja pekee,” adokeza.

Alijiunga na kikosi cha jeshi mwaka wa 1975, na akafuzu tayari kuhudumia Kenya.

Chini ya kipindi cha muda wa miaka mitano aliyochapa kazi, mengi yalitokea.

Moses Gitonga wakati akiwa afisa wa kikosi cha jeshi la Kenya alipata fursa ya kukutana na Mzee Jomo Kenyatta, Rais wa kwanza wa Jamhuri ya Kenya ambapo alimsalimia. Picha/ Sammy Waweru

Gitonga alikuwa mfyatuaji risasi hodari, na alipanda ngazi kuwa Kamanda wa kitengo cha Platuni.

“Miaka miwili na mitatu baadaye, nilipandishwa madaraka na kuwa Kapteni,” Mzee Gitonga asema.

Ni madaraka yaliyojiri kupitia mafunzo ya kipekee katika kikosi cha kijeshi, mitihani na mbinu za uongozi.

Hadi wakati wa kutoka kikosini, kwa kile Gitonga anataja kama kuchukua “staafu ya mapema”, alikuwa amekwea hadi wadhifa wa Luteni.

Ni kufuatia jitihada na bidii ambapo Gitonga aliteuliwa kuwa miongoni mwa maafisa wa kijeshi waliopata mwanya wa kipekee kukutana na Mzee Jomo Kenyatta, ambaye ndiye baba wa Rais wa sasa, Uhuru Muigai Kenyatta.

Baada ya vuguvu la Maumau kuondoa serikali ya Mbeberu, Mzee Jomo Kenyatta alihudumu kama Waziri Mkuu kati ya 1963 – 1964.

Aidha, kati ya 1964 hadi kufariki kwake mwaka wa 1978, alikuwa Rais wa Jamhuri ya Kenya.

“Mzee Jomo Kenyatta alipenda wafanyakazi wenye bidii na waliojotolea katika huduma walizopokezwa,” Gitonga aelezea, akikumbuka alivyokutana na Rais huyo mtangulizi wa Jamhuri ya Kenya.

Vilevile, Gitonga anamtaja Marehemu kama kiongozi aliyethamini amani, utangamano na umoja wa taifa, kando na kuwa Rais aliyetilia mkazo umuhimu wa elimu na kuondoa umaskini katika jamii.

“Alikuwa ameunga misuli, na wakati wa kukusalimia mikononi, ilikuwa ni lazima uwe imara na ngangari,” afisa huyo asema.

Gitonga pia alitangana na Mkuu wa Majeshi enzi hizo, Meja Jenerali Jackson Kimeu Mulinge.

Mkuu huyo wa majeshi pia alihudumu katika serikali ya Rais mstaafu, Daniel Arap Moi, ambaye kwa sasa ni marehemu.

Jenerali Mulinge alifariki mwaka wa 2014 akiwa na umri wa miaka 91.

“Jenerali Mulinge alisaidia kuokoa serikali wakati wa jaribio la kuipindua mwaka 1982,” Gitonga asema, akisisitiza kwamba afisa wa jeshi anapaswa kuwa mkakamavu, jasiri na mwenye bidii.

Mbali na kupandishwa madaraka, Gitonga pia alipata tuzo ainati, ikiwemo kombe la hadhi.

Ni mkazi wa Gilgil, Kaunti ya Nakuru, na baada ya kuondoka serikalini aliingilia shughuli za kilimo na ufugaji.

Isitoshe, ni mwanaharakati, mtetezi wa haki za wanyonge, ambapo anafichua si kesi moja, mbili au tatu amewasilisha kortini kutetea maslahi ya wananchi na pia vipande vya ardhi ya umma iliyonyakuliwa kuona kwamba ardhi hiyo inarejeshwa.

“Kuna baadhi ya kesi ambazo nimeshinda, na nyingine nyingi zingali zinaendelea kusikilizwa,” Mzee Gitonga asema.

You can share this post!

Wakenya ‘wasukuma’ juu bei ya mafuta TZ

Fisi aibiwa tairi akila vya haramu