• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
MARY WANGARI: Wazazi watumie likizo kuwapa watoto malezi bora

MARY WANGARI: Wazazi watumie likizo kuwapa watoto malezi bora

Na MARY WANGARI

SHULE nyingi zilifunguliwa jana baada ya wanafunzi kuwa nyumbani kwa likizo ya zaidi ya mwezi mmoja.

Hata hivyo, wanafunzi wa madarasa mengine wakirejea shuleni, wenzao wa Gredi ya Nne watasalian nyumbani hadi Julai. Waliofanya mtihani wa Darasa la Nane piawatakuwa nyumbani wakisubiri kujua shule watakazopata ili kujiunga na elimu ya sekondati.

Hali hii ya kuwa na baadhi ya wanafunzi ambao watakuwa nyumbani wenzao wakiendelea na masomo, limeibua wasiwasi na minung’uno miongoni mwa wazazi na walezi.

Hii ni baada ya kuzuka kwa janga la Covid-19 ambalo lilivuruga mifumo ya elimu duniani huku wanafunzi nchini Kenya wakilazimika kukaa nyumbani kwa kipindi cha miezi 10.

Likizo hiyo ndefu haikukosa madhara yake huku ikiacha athari za kudumu kwa baadhi ya watoto.Kuanzia matumizi ya mihadarati, kujihusisha na ngono, mimba za mapema, hadi uhalifu, ni miongoni tu mwa maovu yaliyojitokeza katika likizo hiyo.

Baadhi wakiwa wamekata tamaa ya kurejea shule, wengine walianza kusaka riziki na hata kugeukia uendeshaji bodaboda na kuzika elimu katika kaburi la sahau.

Kwa wengine, hasa wasichana, ndoto ya kurejelea masomo yao ilitokomea kabisa huku wakiwa wahasiriwa wakuu wa dhuluma za kingono, mimba na ndoa za mapema.

Pia kulikuwa na athari za kiafya na kisaikolojia kutokana na watoto kutumia muda mwingi wakitazama televisheni, mitandao ya kijamii badala ya kucheza na kutangamana na wenzao.

Si ajabu kwamba wazazi na walezi wanahofia kuwa athari hizo huenda zikajitokeza tena kwa wanafunzi walioagizwa kuendelea kukaa nyumbani kwa muda zaidi.

Hata hivyo, kipindi cha likizo vilevile kina manufaa yake hasa kwa kuimarisha uhusiano kati ya wazazi na watoto wao.Kando na kukatiza shughuli za elimu, likizo ndefu iliyosababishwa na virusi hatari vya corona, ilidhihirisha wazi jinsi wazazi walivyotelekeza majukumu yao ya malezi na kuwaachia walimu kazi yote.

Si ajabu basi baadhi ya wazazi na walezi waligutushwa na uhalisia mchungu kwamba hawafahamu chochote kuhusu watoto wao wenyewe.

Matokeo yake yalikuwa kuongezeka kwa visa vya utovu wa nidhamu kwa watoto na visanga vya kila aina vilivyowaacha Wakenya vinywa wazi.

Likizo hutoa fursa muhimu kwa wazazi kuwa kielelezo bora kwa watoto wao, kuwashauri na kuimarisha uhusiano kati yao kwa kushiriki muda pamoja.

Pamoja na kuwasaidia kudurusu masomo waliyofunzwa shuleni, wazazi pia wanaweza kuwasaidia kujihami vilivyo kukabiliana na maisha kwa jumla kwa kutumia maarifa na tajriba zao binafsi.

You can share this post!

Bandari: Wachukuzi watoa masharti kwa serikali

CECIL ODONGO: Wandani wa Ruto Mlima Kenya wamemgeuka?