• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 4:40 PM
MAWAIDHA YA KIISLAMU: Waislamu walinde umoja, undugu kulingana na mafunzo ya kidini

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Waislamu walinde umoja, undugu kulingana na mafunzo ya kidini

Na HAWA ALI

SIFA zote njema anastahiki Mola Azzawajalla.

Swala na salamu anastahiki Mtume Muhammad Swallallahu Alayhi Wasallam maswahaba wake watukufu na watangu wema hadi Siku ya Kiyaamah.

Suala la umoja katika umma wa Kiislamu, ni jambo lenye umuhimu mkubwa na ambalo limesisitizwa sana katika Qur’ani na Hadithi za Mtume Swallallahu Alayhi Wasallam. Kinsingi ni kuwa umoja ni nguzo muhimu katika mafundisho ya Qur’ani na pia unachukuliwa kuwa moja ya misingi muhimu katika Hadithi za Mtume Muhammad Swallallahu Alayhi Wasallam

Qur’ani Tukufu inauchukulia umoja kuwa neema kubwa na maalumu na kumchukulia Mwenyezi Mungu kuwa sehemu muhimu na ya msingi katika kupatikana umoja huo.

Inawataka Waislamu na waumini kutafakari na kukumbuka historia chungu ya mgawanyiko na ghasia na kufanya juhudi za kulinda umoja wao, kwa sababu kuwepo umoja kati ya umma na waumini ni takwa muhimu la Mwenyezi Mungu.

Qur’ani Tukufu inazitaja zama za ujahilia kuwa zama za mifarakano na hitilafu, zama ambazo baadaye zilibadilika na kuwa zama za umoja na kuhurumiana kutokana na neema ya Uislamu.

Aya ya 103 ya Surat Aal Imran inasema: Na shikamaneni na Kamba ya Mwenyezi Mungu nyote wala msifarikiane. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu juu yenu mlipokuwa maadui nyinyi kwa nyinyi, naye akaziunganisha nyoyo zenu; kwa neema yake mkawa ndugu.

Kwa mtazamo wa Uislamu, ulimwengu umejengeka kwa msingi wa Tauhidi na umoja. Kutokana na kuwa Tauhidi ni jambo la kimaumbile, Waislamu wote wanalienzi jambo hilo na kwa hakika ndio msingi muhimu zaidi unaounganisha madhehebu yote ya Kiislamu, na dini zote za Mwenyezi Mungu. Kumwamini Mwenyezi Mungu mmoja huunganisha nyoyo za waumini na kuwafanya kuhurumiana na kushirikiana, ni kana kwamba wote wana moyo mmoja.

Aya ya 92 ya Surat al-Anbiyaa inasema: Kwa hakika huu umma wenu ni umma mmoja, na Mimi ni Mola wenu kwa hivyo niabuduni Mimi.

Kwa mujibu wa wafasiri wa Qur’ani Tukufu, maana ya umma mmoja ni umma ambao hauitilafiani na wote kuwa na neno moja kwa msingi wa Tauhidi. Hata hivyo tunapasa kuashiria hapa nukta hii muhimu kwamba hata kama umoja ni jambo la kimaumbile lakini linahitajia malezi na uzingatiaji maalumu, la sivyo, haliwezi kustawi kama inavyotakikana na huenda likakabiliwa na hatari ya kupotoshwa.

Undugu wa kidini au Kiislamu ambao unatajwa mara kwa mara katika Qur’ani una athari kubwa katika kuimarisha na kuleta umoja na mshikamano katika umma wa Kiislamu.

Undugu huo wa kidini na Kiislamu umetajwa katika Aya nyingi za Qur’ani kuwa nguzo muhimu inayoeneza umoja wa Waislamu na kupambana na kila aina ya mifarakano na unafiki. Baada ya kuashiria kanuni hiyo kuu katika Surat Hujuraat, Mwenyezi Mungu anasema katika Aya ya 9 ya Sura hiyo: Na ikiwa makundi mawili katika Waumini yanapigana, basi yapatanisheni. Anasisitiza zaidi suala hili katika Aya inayofuata na kutoa sababu za kuharakishwa jambo hilo kwa kusema: Hakika Waumini ni ndugu, basi patanisheni baina ya ndugu zenu, na mcheni Mwenyezi Mungu ili mrehemewe.

Aya hii inasisitiza kwamba waumini ni ndugu na hivyo wanapasa kuimarisha mapenzi kati yao na kwamba iwapo watatengana basi juhudi zifanyike kwa ajili ya kuwaleta pamoja. Inasema iwapo pande mbili au kadhaa za waumini hao zitagombana na kuhitilafiana basi hatua za haraka zichukuliwe na kundi moja miongoni mwao kwa ajili ya kufanya suluhu na kuzipatanisha pande hizo.

Kama tulivyotangulia kusema, neema ya udugu wa Kiislamu ni neema kubwa zaidi ambayo Mwenyezi Mingu aliwatunuku waumini. Mwenyezi Mungu anazungumzia tena neema hiyo katika Aya ya 63 ya Surat Anfaal kwa kusema: Na akaziunganisha nyoyo zao. Na lau wewe ungelitoa yote yaliyomo duniani usingeliweza kuziunganisha nyoyo zao, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaunganisha. Hakika Yeye ndiye Mtukufu Mwenye nguvu na Mwenye hekima.

Katika jamii ambayo ina makundi tofauti ya kimadhehebu, mirengo ya kisiasa, kiutamaduni na kadhalika, kuwepo hitilafu miongoni mwa wafuasi wa makundi na mirengo hiyo ni jambo la kawaida kabisa na pia kuwepo mijadala ya kielimu katika nyanja hizo ni jambo la kawaida.

Kwa kawaida hitilafu hizo hutokea katika matawi na sio katika misingi ya imani na itikadi zinazohusiana na masuala hayo, na kwa hivyo hazipasi kuleta mgawanyiko wala kuzuia kupatikana umoja kati ya Waislamu.

Na hasa inapotokea kwamba adui wa Uislamu anapanga njama za kudhoofisha na kuiangamiza jamii ya Kiislamu, Waislamu wote wanapasa kuweka kando tofauti zote za kibinafsi na maslahi ya kimakundi na kufanya jitihada za kuondoa hatari ya pamoja inayowakabili.

Hii ni kwa sababu hitilafu za kimadhehebu na vita vya kikabila huhatarisha usalama wa umma wa Kiislamu na kuzuia kufikiwa malengo yake matukufu. Imam Ali (as) anawatahadharisha Waislamu kutohitilafiana na kutengana katika hotuba ya 176 ya Nahjul Balagha kwa sababu jambo hilo lina madhara makubwa kwa umma wa Kiislamu.

Imam Ali mwenyewe hata kama alikuwa na haki Swallallahu Alayhi Wasallam kutokana na amri iliyotoka kwa Mwenyezi Mungu, lakini alifumbia macho jambo hilo na kutopambana na makhalifa watatu waliotawala kabla yake ili kulinda umoja wa Waislamu. Aliamua kukaa kimya kuhusiana na jambo hilo kwa muda wa miaka 25 laikini pamoja na hayo alikuwa akishirikiana na makhalifa hao alipohitajika kufanya hivyo kwa lengo la kulinda umoja na maslahi makuu ya umma wa Kiislamu. Hii ni kwa sababu baada ya kuaga dunia Mtume (saw) kulidhihiri manabii wa uongo katika umma wa Kiislamu ambao walisababisha migogoro mikubwa katika jamii na hata kuwafanya baadhi ya watu waliokuwa wamesilimu karibuni kuritadi na kurudi katika imani zao potovu za zamani.

You can share this post!

Covid: Wanaohepa chanjo kuadhibiwa

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Rais Uhuru alionyesha heshima kubwa...