• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
MBWEMBWE: Guu la kushoto la Mahrez linazidi kumvunia dhahabu

MBWEMBWE: Guu la kushoto la Mahrez linazidi kumvunia dhahabu

Na CHRIS ADUNGO

RIYAD Karim Mahrez, 30, ni winga matata raia wa Algeria ambaye kwa sasa anasakata soka ya kulipwa kambini mwa Manchester City – mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

Alijitosa katika ulingo wa soka akivalia jezi ya kikosi cha AAS Sarcelles nchini Ufaransa, kabla kusajiliwa na klabu ya Quimper mnamo 2009.

Alichezea timu hiyo msimu mmoja pekee akahamia Le Harve kwa miaka mitatu.Ilikuwa hadi Januari 2014 ambapo Mahrez aliingia katika sajili rasmi ya Leicester City.

Akawa sehemu ya kikosi kilichoshindia klabu hiyo taji la Ligi ya Daraja ya Kwanza nchini Uingereza (Championship) mwishoni mwa mwaka huo, na hivyo kufuzu kwa kipute cha EPL.

Mwishoni mwa msimu 2015-16, Mahrez alitawazwa Mchezaji Bora wa Mwaka nchini Algeria. Alituzwa pia taji la PFA la Mchezaji Bora wa Mwaka na akatiwa katika Kikosi Bora cha Mwaka cha PFA, baada ya kuongoza waajiri wake kunyanyua ubingwa wa EPL.

Mwaka 2018 sogora huyo mwenye guu kali la kushoto alijiunga na Man-City. Alisaidia klabu hiyo kushinda ufalme wa EPL, Kombe la FA na taji la EFL Cup katika msimu wake wa kwanza ugani Etihad.

Ingawa alizaliwa Sarcelles nchini Ufaransa, Mahrez aliteua kuchezea timu ya taifa ya Algeria iliyomwajibisha kwa mara ya kwanza mnamo 2014.

Aliwakilisha kikosi hicho kwenye Kombe la Dunia 2014 nchini Brazil kisha Kombe la Afrika (AFCON) 2015, 2017 na 2019.

Algeria walinyanyua ubingwa wa AFCON mnamo 2019 nchini Misri chini ya unahodha wa Mahrez, aliyetawazwa na Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) kuwa Mchezaji Bora wa Afrika 2016.

Babake Mahrez, Ahmed, alikuwa mzawa wa Algeria wa eneo la Beni, Snous katika wilaya ya Tlemcen naye mamake ana usuli wa Algeria na Morocco.

Babake Mahrez aliwahi kucheza soka nchini Algeria na aliaga dunia kutokana na mshtuko wa moyo Mahrez akiwa na umri wa miaka 15 pekee.

UKWASI

Mahrez yuko katika kundi la tatu la masogora wanaodumishwa kwa mshahara mnono zaidi ugani Etihad.

Ujira wake wa Sh78 milioni kila mwezi unawiana na ule wa Rodrigo Hernandez na Aymeric Laporte.

Wanasoma kwa karibu migongo ya Ilkay Gundogan, Bernardo Silva na Fernandinho Luis Roza.

Wanasoka wanaotia mfukoni kiasi kikubwa zaidi cha mshahara kikosini Man-City ni Kevin De Bruyne, Raheem Sterling na Jack Grealish.

Akiwa Leicester, Mahrez alikuwa akitia mfukoni mshahara wa Sh10 milioni. Kufikia mwisho wa Juni 2021, thamani ya mali ya Mahrez ilikadiriwa kufikia kima cha Sh4.6 bilioni.

Winga Riyad Mahrez wa Man-City katika mechi ya awali ugani Etihad. Picha/Maktaba

Jarida la Forbes lilimweka nambari 72 miongoni mwa masogora wanaovuna hela nyingi zaidi ulingo wa soka.

Ilivyo, fowadi huyu hupokea ujira wa takriban Sh1 bilioni kwa mwaka pamoja na nyongeza ya Sh365 milioni kwa kuwa balozi wa mauzo ya bidhaa na huduma za kampuni ya Nike.

Isitoshe, hujirinia marupurupu na bonasi tele akisajili sare au ushindi mechi za klabu na timu ya taifa au kuvuna ushindi katika vibarua tofauti kwenye ngazi ya klabu na timu ya taifa.

Mahrez pia hufanya matangazo mengi kwa ajili ya kuvumisha huduma na bidhaa za kampuni mbalimbali ambazo humlipa kitita kinono kwa mujibu wa maelewano.

MAGARI

Kwa mwanasoka wa kiwango na haiba yake, Mahrez huvutiwa zaidi na michuma ya kisasa inayohusishwa na mwendo wa kasi.

Baadhi ya magari anayoyamiliki ni pamoja na Aston Martin, Ferrari F12 TDF, Audi Q9 Ferrari, Porshe na Lamborghini Gran-Turismo ambayo kwa pamoja yanakisiwa kumgharimu kima cha Sh106 milioni.Mchumba wake kwa sasa, Taylor Ward, huendesha magari aina ya Wrangler S-SUV na Range Rover ambayo yanakisiwa kumgharimu Mahrez Sh70 milioni.

MAJENGO

Moja kati ya makasri yanayomilikiwa na Mahrez nchini Uingereza ni la Sh620 milioni jijini Manchester anakoishi na familia yake. Mnamo 2017, alijinunulia jengo jingine la Sh540 milioni jijini Algiers, Algeria ambako amewekeza sana katika sekta ya kilimo, vipuri vya magari na bidhaa za utabibu.

FAMILIA NA MAPENZI

Mahrez alizaliwa katika mnamo Februari 21, 1991.

Alifunga pingu za maisha na kipusa Rita Johal mnamo 2015 na wakajaliwa mtoto wa kike mwaka uliofuata. Mnamo Juni 2019, wakiwa na watoto wawili wa kike, Mahrez na Rita walipatikana na hatia ya kutomlipa yaya wao wa awali na wakaagizwa na mahakama moja nchini Uingereza kumfidia Sh562,000.

Mahrez alianza kutoka kimapenzi na Taylor mnamo Oktoba 2020 baada ya kutemana na Rita naye kipusa huyo kutengana na mwanasoka Sergio Aguero ambaye sasa anachezea Barcelona.

Ili kudhihirisha ukubwa wa kiwango cha kukomaa kwa penzi kati yake na Taylor, 23, Mahrez alimvisha kidosho huyo pete ya almasi ambayo thamani yake inakadiriwa kuwa Sh62 milioni mnamo Juni 21, 2021.

Nyota huyo aliyepatikana na virusi vya corona mnamo Septemba 7, 2020, alipoteza vito vya thamani kubwa pamoja na kiasi kisichojulikana cha pesa mnamo Mei 2020 baada ya kasri lake jijini Manchester kuvamiwa na majambazi waliompora.

Kwa mujibu wa Rita ambaye ni mwanamuziki, hatua ya Mahrez kujiunga na Man-City ilichangia kusambaratika kwa ndoa yao.

“Mahrez ambaye awali alikuwa mnyenyekevu kiasi cha hata kuwa radhi kutumwa sokoni kununua mboga akiwa Leicester, alibadilika ghafla na kuwa jeuri baada ya kiburi cha kuvalia jezi za Man-City kumuingia kichwani,” akaungama.

“Mahrez hakuwa tena akishikika baada ya Man-City kuanza kumpokeza mamilioni yasiyohesabiki kila baada ya wiki,” akaongeza Rita, 28.

“Mahrez alikubali umaarufu umtawale. Alibadilika sana akawa haambiliki hasemezeki. Alisahau kwamba nilisilimu na kuacha maisha ya anasa – ya kunywa pombe na kutoka kimapenzi na mabwanyenye zaidi yake kwa ajili ya kudumisha uhusiano wangu naye.”

Japo walidumu katika ndoa kwa miaka saba, Rita ameshikilia kwamba Mahrez alianza kuwa na mienendo isiyoelekewa pindi baada ya kuhamia Man-City kwa Sh8.4 bilioni mnamo 2018.

Rita ambaye amewahi kuigiza katika filamu za Kingsman: The Secret Service na Cinderella alianza kumfungulia Mahrez mzinga wake wa asali mnamo 2014.

You can share this post!

UDAKU: Ma’ Rashford mbioni kupatanisha mwanawe na mrembo...

DIMBA NYANJANI: Amazon Tigers shabaha yao kunogesha Ligi...