• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 8:55 PM
UDAKU: Ma’ Rashford mbioni kupatanisha mwanawe na mrembo Lucia Loi

UDAKU: Ma’ Rashford mbioni kupatanisha mwanawe na mrembo Lucia Loi

Na CHRIS ADUNGO

MSHAMBULIAJI mahiri wa Manchester United, Marcus Rashford, yu mbioni kurudiana na mchumba wake wa tangu utotoni, Lucia Loi.

Videge hao walitemana mwezi Mei baada ya kudumu katika uhusiano wa kimapenzi kwa kipindi cha miaka minane.

“Rashford hajawahi kupata utulivu tangu atengane na Lucia. Anaumia sana kimawazo tangu wakati huo. Kinachomkoroga nyongo ni hatua ya Lucia kufuta picha zao zote mitandaoni baada ya kufunganya virago kwenda zake,” akatanguliza msemaji wa familia ya Rashford, 23.

“Bila shaka walitofautiana kuhusu mambo fulani. Lakini kutengana kwao hakukuhusisha mtu yeyote. Waliachana kwa amani na sasa wanapania kurudiana sababu mamake Rashford, Melanie Maynard, amejitolea kuwapatanisha. Bado wanawasiliana. Walipendana na kustahiana sana. Wangali wachanga na walikuwa katika mwanzo wa safari ambayo ingeishia kwa ndoa,” aliongeza.

Lucia, 23, ni afisa wa mahusiano mema katika kampuni moja ya sukari nchini Uingereza.

Alikuwa nguzo muhimu katika safari ya kuimarika kwa Rashford kitaaluma hadi akawa mshambuliaji tegemeo kambini mwa Man-United na timu ya taifa ya Uingereza.

Kwa mujibu wa Melanie, ambaye amekuwa akimhimiza mwanawe kufunga pingu za maisha na Lucia, kiini cha kusambaratika kwa uhusiano wao ni presha iliyochangiwa na masharti makali, hasa ya ‘lockdown’ nchini Uingereza katika juhudi za kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona.

Lucia, ambaye amefanya kazi nyingi za hisani nchini Zambia na Sri Lanka, amekuwa akiunga mkono miradi mingi ya Rashford, ambaye amekuwa akipigana dhidi ya umaskini na kutetea haki za watoto kupata mlo na elimu.

Hisani hiyo ilimfanya staa huyo kupewa tuzo ya Member of the Order of the British Empire (MBE) mnamo Oktoba 2020, na akatiwa kwenye orodha ya waheshimiwa watakaokuwa wakihudhuria maadhimisho ya siku ya kuzaliwa ya Malkia wa Uingereza.

“Japo wametengana bado kuna mapenzi ya dhati kati yao. Wanastahili kuzungumziwa na mtu atakayewaelewesha kuhusu pandashuka za kawaida maishani,” akasema mmoja wa marafiki wakuu wa Rashford aliyenukuliwa na gazeti la The Sun.

Aliongeza rafiki huyo: “Ni vizuri kwamba juhudi hizo za kuwapatanisha zimeshika kasi. Tutarajie makuu hivi karibuni kisha harusi baadaye mwaka huu au mapema mwakani.”

Rashford alianza kutoka kimapenzi na Lucia mnamo 2013 wakiwa wanafunzi Shule ya Mersey, eneo la Ashton jijini Manchester.

Sogora huyo ndiye kitinda mimba katika familia ya watoto watano waliolelewa na mzazi mmoja – Melanie, katika eneo la Wythenshawe jijini Manchester.

Alianza kuvalia jezi za kikosi cha kwanza cha Man-United mnamo 2016 akiwa na umri wa miaka 18 pekee na akafunga mabao mawili dhidi ya Arsenal katika mchuano wake wa kwanza.

Miaka miwili baadaye, alitiwa kwenye kikosi kilichotegemewa na Uingereza katika fainali za Kombe la Dunia nchini Urusi mnamo 2018.

Lucia alihudhuria mechi zote zilizosakatwa na Uingereza kwenye fainali hizo huku akivalia jezi zilizoandikwa jina Rashford mgongoni.

Rashford alifungia Man-United jumla ya mabao 19 katika mapambano yote msimu jana.

Aliwaongoza waajiri wake kukamilisha kampeni za Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) katika nafasi ya pili na kutinga fainali ya Europa League dhidi ya Villarreal ya Uhispania.

Rashford alirejelea mazoezi kambini mwa Man-United kwa mnamo Ijumaa iliyopita baada ya kufanyiwa upasuaji kwenye bega.

Hajawajibishwa katika mchuano wowote tangu aletwe uwanjani katika kipindi cha pili kwenye fainali ya Euro 2020 iliyokutanisha Uingereza na Italia mnamo Julai 11.

You can share this post!

Brighton na Arsenal waumiza nyasi bure katika mechi ya EPL...

MBWEMBWE: Guu la kushoto la Mahrez linazidi kumvunia dhahabu