• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 1:15 PM
MUTUA: Mwafrika amejihini na kujitweza mwenyewe

MUTUA: Mwafrika amejihini na kujitweza mwenyewe

Na DOUGLAS MUTUA

MWAFRIKA akiwajibishwa na Mzungu hupiga kamsa na kudai anaonewa, ati msingi wa maonevu ni ubaguzi wa rangi pekee.

Madai rahisi kuaminika hayo na wasiokwangura mambo wakajua mmejificha nini msimoonekana mara moja.

Imekuwa desturi yetu tangu enzi za mkoloni kwa kuwa aghalabu hatutaki kukiri kwamba tuna matatizo ya kimsingi yanayotuhini ila hatuwezi kujizuia.

Na hatutaki kubadilika.

Kelele za kila nui zilihanikiza hewani kote barani hivi majuzi Uingereza iliposimama kidete kukatalia mbali ithibati zinazotokea Afrika zikionyesha watu wamepata chanjo za corona.

Msimamo huo wa Uingereza una maana kwamba hata ukiwasilisha cheti chako kinachothibitisha umepata chanjo zote mbili, mradi umechanjiwa Afrika, hakikubaliki.

Ama utazuiwa kuingia Uingereza au utaruhusiwa kisha ufungiwe katika hoteli maalum kwa siku 14.

Ukiwa humo utapimwa mara mbili ili kuhakikisha kabisa huna korona.

Ni Wakenya na Wamisri pekee ambao wataruhusiwa kujifungia kwa muda huo wanakonuia kukaa wakiwa Uingereza, lakini wao pia lazima wapimwe mara mbili.

Agizo hilo lilitolewa mapema wiki jana Uingereza ilipotangaza orodha mpya ya mataifa ambayo yataruhusiwa kuingia humo kwa masharti nafuu kuliko awali.

Ililegezea masharti hayo jumla ya mataifa 70, lakini bara zima la Afrika lilizimwa. Haingii mtu Uingereza kwa raha zake ati!

Agizo lenyewe lilionekana kukinzana na uhalisia wa mambo kwa kuwa Uingereza imetuma mamilioni ya chanjo hizo Afrika.

Swali kuu ni je, kwani ilitutumia chanjo dhaifu ambazo yenyewe haina imani nazo? Huenda zilikuwa bandia?

Maswali hayo yanawatia hofu wanaowahamasisha watu kuhusu umuhimu wa kupata chanjo wakati huu ambapo korona inaendelea kuangamiza.

Kisa na maana ni kwamba hata bila tangazo hilo, kuna watu wengi mno wasioziamini chanjo hizo, hivyo huko ni kutia msumari moto kwenye kidonda.

Wataziamini kamwe?

Hadi hapo, huo ndio ukweli finyu anaotaka kushikilia Mwafrika anayeamini anaonewa kwa misingi ya rangi yake.

Ametia pamba masikioni, maelezo ya ziada hataki.

Hata hivyo, ukweli wa mambo ni kwamba Mwafrika akichanjiwa kwenye mataifa ambayo yanaaminiwa na Uingereza hatazuiwa kuingia taifa hilo.

Tayari, hapo unaona kuwa tatizo si rangi ya anayejaribu kuingia Uingereza bali aliyemchanja.Kumbuka Mwingereza anatujua vizuri: akitupa msaada wa chanjo tunaweza kuuuza na kutia chupa zake maji kisha tukadanganya chanjo yake hiyo na kuwapa watu.

Anajua pia tuna uwezo wa kughushi vyeti vya kuthibitisha tumechanjwa kisha tukaviwasilisha kwake bila kupepesa macho tukitaka kuingia Uingereza na virusi mwilini.

Hivi tumeghushi shahada za vyuo vikuu kufikia uzamifu, karatasi duni ya chanjo itatushinda wapi?

Ni Afrika pekee ambako unasikia kesi za ajabu kama vile mzee mzima na mvi zake kusimama mahakamani na kukaa kimya akisubiri jaji aamue mzee ana digrii au la.

Ikiwa mzee hana, mbona mwenyewe asiseme mara moja hana? Angekuwa mkweli na mwadilifu, mwanzo kesi yenyewe haingekuwapo!

Walionunua digrii Uganda bila kusoma hata siku moja wakaishia kuchaguliwa magavana na kugeuka vingang’anizi katika suala zima la ‘ninayo – hunayo’ unawajua.

Pia walioghushi digrii za vyuo vikuu vya nchini Kenya wakawa magavana, pekuzi za kina zilipotishia kuwasomba wakakimbilia kwa vigogo kutakaswa na kukingwa unawajua.

Ni Afrika pekee ambako mradi ana mafedha, mtu ataghushi cheti cha kifo chake ili atoroke jela, ausadikishe umma umchague, kisha akivuruga mambo ajisingizie Ukimwi ili asifungwe!

Ni Afrika pekee ambako viongozi hutajirika kuliko mataifa wanayoongoza, na kwa kuwa hawaziamini serikali zao hizo wanachimba mashimo ughaibuni na kufukia mafedha hayo!

Ili atie akili, Mwafrika anahitaji kuwekewa vikwazo vya kumuumiza na kumtenga na ulimwengu wa wastaarabu. Huko ndiko kumzuia mtu kujihini mwenyewe. Kunafaa.

[email protected]

You can share this post!

KAMAU: Kenya iziige nchi nyingine duniani kulinda tamaduni...

Ronaldo afikia rekodi ya Rooney ya kutawazwa Mchezaji Bora...