NA CHRIS ADUNGO
WANAFUNZI wanahitaji mazoezi mengi iwezekanavyo ili wajiamini katika usomaji na ujifunzaji wa dhana mpya.
Njia rahisi ya kukuza uwezo wao wa kuhusisha wanachokisoma darasani na matukio ya kawaida katika jamii, ni kuwashirikisha katika usomaji wa mara kwa mara na usimulizi wa hadithi.
Michezo, nyimbo na mashairi mepesi ambayo wanafunzi waweza kuyaimba kwa urahisi, yanasaidia pia kujenga mahusiano hayo.
Haya ni kwa mujibu wa Bw Charles Otieno Onyango ambaye kwa sasa ni mwalimu wa Kiingereza na somo la Dini katika shule ya msingi ya Holy Cross St James Dandora, Kaunti ya Nairobi.
“Jukumu kubwa la mwalimu ni kuamsha ari ya wanafunzi katika kusoma na kuandikamizike zaidi katika stadi hizo. Tunga mashairi mepesi ambayo watayakumbuka haraka. Waimbe nyimbo kwa kuonyesha vitendo wanapocheza. Kusoma kwa namna hii kunasisimua na kuchangamsha,” anasema.
Kwa mtazamo wa mwalimu Otieno, uzuri wa kufundisha watoto wa umri mdogo – wa kiwango cha shule za msingi – ni kwamba wanaelewa mambo upesi na wana hamu ya kujifunza vitu vipya mara kwa mara.
Otieno alizaliwa katika eneo la Juja, Kaunti ya Kiambu na akalelewa katika eneo la Ugunja, Kaunti ya Siaya. Ndiye wa pili katika familia ya watoto sita wa Bw Titus Onyango na Bi Margaret Anyango.
Alianza safari ya elimu katika shule ya msingi ya Umina, Siaya (1995-2002) kabla ya kujiunga na shule ya upili ya Barding, Siaya (2003-2006). Ingawa alitamani kuwa mwanahabari, alisomea masuala ya bima, mauzo pamoja na uvumishaji wa bidhaa na huduma katika eneo la Nyahururu, Kaunti ya Nyandarua (2007-2009).
Alifanya kazi ya kuuza bima katika maeneo mbalimbali ya Kaunti za Mombasa, Kwale na Kilifi kabla ya kujiunga na Chuo cha Mafunzo ya Ualimu cha Machakos (2009-2012). Alisomea pia masuala ya ushauri nasaha katika chuo kimoja jijini Nairobi na akafuzu mwaka wa 2013.
Baada ya kuhitimu ualimu, Otieno alianza kufundisha Kiswahili katika shule ya Sirembe, Siaya, mnamo 2012. Alihudumu huko kwa mwaka mmoja kabla ya kujiunga na Maasai Group of Schools, Kajiado, alikofundisha Kiswahili na somo la Dini hadi mwisho wa 2014.
Onyango amewahi pia kufundisha katika shule ya msingi ya PCEA Kariobangi South, Nairobi, (2016-2022) baada ya kuwa Mwalimu Mkuu katika shule ya Nile Basin, Kajiado, hadi Mei 2016. Alijiunga na shule ya Holy Cross St James Dandora mnamo Februari 2022.
Kadri anavyolenga kujiendeleza kitaaluma kwa kusomea shahada ya ualimu, kubwa zaidi katika malengo ya Onyango ni kuwa mshauri nasaha na mwandishi maarufu wa vitabu vya kufundishia Mtaala wa Umilisi (CBC).
Kati ya mambo yaliyochangia umilisi wake wa Kiswahili ni ulazima wa kutumia lugha hii kuwasiliana na watu wa jamii na matabaka mbalimbali katika maeneo alimokulia. Onyango anatambua pia ukubwa na upekee wa mchango wa kaka yake, Bw Nicholas Ochieng, katika kumhimiza kuchapukia masomo ya lugha na hatimaye kujitosa katika ulingo wa ualimu.
Bw Ochieng kwa sasa anafundisha Kiingereza katika shule moja ya sekondari iliyoko Siaya. Ndiye anazidi kumpa Onyango motisha ya kupiga mbizi katika bahari ya utunzi wa vitabu na kumpigia mhuri wa kuwa mwalimu bora wa Kiswahili.
Subscribe our newsletter to stay updated