Na CHRIS ADUNGO
PAMOJA na kutumia vifaa vya kidijitali ambavyo husisimua wanafunzi, matumizi ya video, michoro na picha za rangi kupitia kompyuta ni namna nyingine ya kufanya masomo kuwa ya kuvutia.
Kwa mujibu wa Bw Martin Gitonga, mwanafunzi akipata umilisi na ujuzi unaofaa, atakuwa wa manufaa sana katika jamii ya sasa inayoshuhudia mabadiliko ya kasi ya kiteknolojia katika takriban sekta zote.
Kutokana na ukweli huu, ipo haja kwa walimu kukumbatia matumizi ya mbinu anuwai za ufundishaji zitakazompa mwanafunzi nafasi murua ya kushiriki shughuli za ujifunzaji kikamilifu.
“Kuhusisha wanafunzi moja kwa moja katika masomo yanayohitaji ubunifu wa kiteknolojia kunawapa fursa ya kufanya mambo kwa kujiamini. Mawanda ya fikira zao hupanuka, uelewa wao huimarika na huanza kuona vitu wanavyofundishwa vikiwa vya kawaida mno,” anasema Bw Gitonga.
“Hali hii huchochea bongo zao kufanya kazi na hatimaye maarifa wanayoyachota vitabuni na kutoka kwa walimu wao yataamsha hamu ya uvumbuzi ndani yao,” anaelezea.
Gitonga almaarufu ‘Malenga wa Bara’ ni mtaalamu wa kufundisha Kiswahili mitandaoni. Alizaliwa katika kijiji cha Iriga, eneo la Muthambi, Kaunti ya Tharaka Nithi. Ndiye kifungua mimba katika familia ya watoto wawili wa Bw Jasper Gitonga na Bi Harriet Kanyua.
Alianza safari ya elimu katika shule ya msingi ya Gituja, Muthambi (1994-2003) kabla ya kujiunga na shule ya upili ya Muraga, Tharaka Nithi (2004- 2007).
Ingawa alisomea shahada ya uanahabari katika taasisi ya mafunzo ya teknolojia ya habari na mawasiliano ya PAGO jijini Nairobi (2008-2010), alirejea darasani baada ya miaka mingi ili kutimiza ndoto yake ya ualimu.
“Tamaa ya utangazaji iliyeyuka ghafla nilipopata kibarua cha kufundisha Kiswahili katika shule ya upili ya Wiru, Tharaka Nithi (2012). Nilivutiwa sana na uchambuzi wa Fasihi ya Kiswahili. Awali, nilikuwa nimefundisha katika shule ya upili ya Muraga Girls (2008) kabla ya kujiunga na PAGO,” anasema.
Kwa kuwa alama alizokuwa amejizolea katika KCSE 2007 zilimkosesha nafasi ya kusomea ualimu katika chuo kikuu, alihiari kurudi sekondari baada ya miaka sita na akajiunga na shule ya upili ya Gikurune Boys, Kaunti ya Meru akiwa mwanafunzi wa kidato cha tatu mnamo 2013.
Alifaulu vyema katika KCSE 2014 na akasomea shahada ya ualimu (Kiswahili/Dini) katika Chuo Kikuu cha Kenyatta kuanzia 2015. Baada ya kuhitimu, alifundisha katika shule ya upili ya Katheri Boys, Meru hadi 2021.
Aliwahi pia kusomea kozi ya Umilisi wa Taaluma ya Kiswahili katika Kituo cha WASTA, Matasia, Ngong mnamo Oktoba 2010.
Mbali na ualimu, Gitonga pia ni mfawidhi wa sherehe muhimu za watu binafsi, mashirika, kampuni na idara mbalimbali za serikali.
Ufanisi huo ni zao la kipaji chake cha ulumbi, weledi wa kusarifu lugha, upevu wa masimulizi na ujuzi alio nao katika kuremba na kusuka maneno kiufundi.
Aliwahi kuwa mratibu wa mawasiliano katika ofisi ya aliyekuwa Mbunge Mwakilishi wa Wanawake katika Kaunti ya Tharaka Nithi, Beatrice Nkatha kati ya 2016 na 2018.
Alianza kufundisha Kiswahili mitandaoni baada ya janga la korona kubisha humu nchini mwanzoni mwa 2020.
“Nilianzisha chaneli ya YouTube, ‘Kiswahili na Bin Gitonga’ iliyoziba pengo la ufundishaji wa Kiswahili nchini,” anasema.
Kwa kutumia kipaji chake cha uandishi, amepiga hatua kubwa kutokana na upekee wake wa kuoanisha talanta, maarifa ya kiteknolojia na taaluma alizozisomea.
Kubwa zaidi katika maazimio yake ni kuwa miongoni mwa walimu watakaobadilisha sura ya ufundishaji na ujifunzaji wa Kiswahili kiteknolojia katika enzi hii ya utandawazi.
Subscribe our newsletter to stay updated