NA ENOCK NYARIKI
MIONGONI mwa maneno ambayo hukosewa katika mawasiliano ni ‘miongoni mwa’.
Baadhi ya watu wana mazoea ya kuyatumia maneno hayo pamoja na ‘kama vile’ katika sentensi moja.
Maneno ‘kama vile’ au ‘pamoja na’ hutumiwa mwanzo mwanzo mwa sentensi ili kuashiria kwamba vitu au mambo ambayo yatajitokeza katika usemi ni machache tu kati ya mengi yaliyomo.
Katika sentensi iliyotangulia hii, nimetumia maneno ‘kati ya mengi’ kwa maana ile ile ya ‘miongoni mwa’.
Waama, iwapo mzunguzaji ametumia maneno ‘kama vile’ au ‘kwa mfano’ katika sentensi yake, hapaswi tena kuikamilisha sentensi hiyo kwa ‘miongoni mwa’.
Kwa mfano: *Mambo yanayosababisha ukatili wa kimatendo ni kama vile wizi na unyang’anyi; unyanyasaji wa kimapenzi na uharibifu wa mali miongoni mwa mengine.
Kosa la uradidi usiokuwa na maana linajitokeza katika sentensi hii kutokana na kukamilishwa kwa ‘miongoni mwa mengine’.
Tulivyoeleza hapo juu ni kwamba, iwapo tayari mzungumzaji ametaja dhana ‘kama vile’ basi hastahili kutumia miongoni mwa kwa kuwa ile ya kwanza inaashiria uchache.
Kwa msingi huu, sentensi tuliyoitaja hapo juu inapaswa kukosolewa hivi: Mambo yanayosababisha ukatili wa kimatendo ni kama vile wizi na unyang’anyi,unyanyasaji wa kimapenzi na uharibifu wa mali.
Matumizi ya ‘kama vile’ na ‘miongoni mwa’ katika sentensi moja aghalabu hutokea katika maandishi kwa kuwa si rahisi watumiaji wa lugha ya Kiswahili kugundua kuwa kosa hilo limejitokeza.
Alhasili uandishi mzuri unapaswa kutumia iktisadi ya maneno kuwasilisha ujumbe unaotakiwa.
Subscribe our newsletter to stay updated