• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 10:55 AM
NDIVYO SIVYO: Ni kosa kusema ‘gwara’, unafaa kusema ‘paruza’

NDIVYO SIVYO: Ni kosa kusema ‘gwara’, unafaa kusema ‘paruza’

NA NYARIKI NYARIKI

KATIKA makala yaliyotangulia, tuliangazia sababu ambazo yamkini huwafanya watu kutumia neno ‘gwara’ kwa maana ya kumtia mtu alama mwilini kwa kutumia kucha.

Tuliona mchango wa lugha za kwanza za watu katika kuliendeleza neno hilo hivyo.

Mathalani, Wakisii hutumia neno ‘koara’ ambapo tofauti ya kimatumizi baina ya jamii hiyo na ile ya Wakikuyu ni sauti /h/ na /a/.

Wamaragoli hutumia neno ‘kugwarusa’ kwa maana hiyo hiyo. Jambo linalodhihirika bayana ni kukaribiana kimatamshi kwa maneno yanayotokana na lugha tulizozitaja na lile ambalo aghalabu hukosewa katika matumizi.

Tulihitimisha kwa kueleza kwamba upo uwezekano kuwa kiambishi ‘gwa’ kinachojitokeza katika baadhi ya lugha za kwanza hupitia badiliko la kifonolojia na kuwa ‘kwa’ inayojitokeza mwanzoni mwa neno ‘kwaruza’.

Nacho kiambishi {za} mwishoni mwa ‘kwaruza’ ni kile cha kauli ya kutendesha ambacho huchukua sura tofauti katika lugha tulizozitaja.

Alhasili, kumtia mtu alama kwenye ngozi kwa kutumia kucha ni kumparuza. Waama, fasili ya neno hili ni kukwaruza au kukwangura kwa kucha.

Kwa hivyo, mbwa, kuku au paka anapomtia mtu alama mwilini kwa kutumia kucha, tunasema kuwa wanyama hao wamemparuza bali si kumgwara. Hili la pili limetokana na athari za lugha za kwanza za watu.

Kitendo cha kumtia mtu uchungu mwilini kwa kutumia ncha za vidole ni kumfinya bali si kumchuna jinsi baadhi ya watu walivyozoea kusema.

  • Tags

You can share this post!

Lionel Messi afunga mabao mawili na kusaidia Argentina...

Naibu chifu ajivunia usalama katika kaunti ndogo ya Chonyi...

T L