• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 7:53 PM
Ni makosa UN kuzitenga nchi zilizo na misukosuko

Ni makosa UN kuzitenga nchi zilizo na misukosuko

Na WANDERI KAMAU

MIONGONI mwa masuala makuu yanayoonekana kuendelea kuangaziwa pakubwa katika Kongamalo Kuu la Umoja wa Mataifa (UN), nchini Amerika, ni jinsi janga la virusi vya corona lilivyoiathiri dunia.

Wajumbe wengi waliohutubu kufikia sasa kwenye kikao hicho, kikichopangiwa kumalizika Jumatatu ijayo, wameangazia kuhusu haja ya nchi mbalimbali duniani kuungana pamoja ili kukabili athari za janga hilo.

Hata hivyo, suala kubwa ambalo kikao kimeonekana kulisahau ni kutathmini mustakabali wa kiusalama katika nchi zinazokumbwa na misukosuko ya kisiasa kama Afghanistan, Syria, Somalia, Ethipoia kati ya mengine.

Ingawa suala la corona limetikisha chumi za nchi nyingi duniani, kuna haja kubwa washiriki kutathmini mielekeo ya mataifa hayo.

Kwa mfano, taharuki iliyo nchini Afghanistan ilidhihirika wazi baada ya mjumbe aliyekuwa amepangiwa kumwakilisha aliyekuwa rais wa taifa hilo, Ashraf Ghani, kujiondoa katika dakika za mwisho mwisho kwenye orodha ya watu ambao wangelihutubia kongamano hilo.

Mtafaruku huo ulizidishwa na UN kuwanyima nafasi wajumbe wa utawala mpya wa Taliban kuhutubu.Kwenye taarifa kufuatia hatua hiyo, UN ilisema bado haiutambui utawala wa Taliban kama serikali halali iliyochukua mamlaka kwa taratibu zinazokubalika kimataifa.

Bila shaka, tofauti hizo zinaonyesha wazi kuwa kinyume na dhana zilizopo, hali nchini humo si shwari hata kidogo, licha ya wanajeshi wa Amerika kuondoka mwishoni wa Agosti.

Tayari, Taliban wameanza kurejelea baadhi ya masharti ya kiutawala waliyokuwa wakitekeleza katika serikali yao awali, kama kuwanyima wanawake nafasi za kuendelea na masomo yao.

Ikizingatiwa Afghanistan imekuwa likionekana kama ngome kuu ya makundi hatari ya kigaidi kama vile Al-Qaeda, Islamic State (IS) kati ya mengine, kuna haja kubwa UN kuangazia hali ya usalama nchini humo, badala ya kuitenga kwenye shughuli zake muhimu.

Mwelekeo uo huo ndio unaopaswa kuchukuliwa kwa nchi zote zinazokumwa na changamoto za kiusalama.Sababu ni kuwa kwa kuyatenga, UN haijifaidi hata kidogo, bali inahatarisha usalama katika nchi hizo na majirani wake.

Katika mataifa kama Somalia na Ethiopia, changamoto za kiuslama zinazoyaandama zinahatarisha uthabiti wa kisiasa katika nchi kama Kenya, Uganda au Tanzania, kwani ni majirani wake wa karibu.

Hatungependa kuona janga la ugaidi likirejea tena kwa makali yaliyoshuhudiwa awali, kutokana na ukosefu wa umoja na mikakati bora miongoni mwa nchi wanachama wa UN.Umoja pekee ndio utaiwezesha dunia kulishinda janga hilo.

[email protected]

You can share this post!

Mbunge ataka wapewe uhuru kubadilisha hoja za Rais katika...

DOUGLAS MUTUA: Mnyanyaso wa ngono kazini ukabiliwe