• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
ODONGO: Kanu ina kibarua kurejelea umaarufu wake wa awali

ODONGO: Kanu ina kibarua kurejelea umaarufu wake wa awali

Na CECIL ODONGO

CHAMA cha Kanu bado kina safari ndefu kurejelea umaarufu wake wa enzi za utawala wa chama kimoja na miaka ya 90 hata baada ya kumteua mwenyekiti wake Gideon Moi kuwania Urais mwakani.

Wajumbe 3,000 wa Kanu mnamo Alhamisi wiki jana waliandaa Kongamano katika ukumbi wa Bomas ambapo seneta wa Baringo aliidhinishwa kugombea Urais mwaka 2022.

Wengi walinasibisha kongamano hilo na lile la 2002 ambalo liliidhinisha Uhuru Kenyatta kuwania kiti cha Urais wakati Daniel Arap Moi alikuwa akistaafu baada ya miaka 24 uongozini. Rais wa Pili wa Kenya alifariki Februari 2020.

Hata hivyo, ni jambo lisilofichika kuwa chama hicho kimesalia kigae na itabidi kijikaze kisabuni iwapo kina nia ya kurejelea umaarufu huo.

Ni vyema ifahimike kwamba wakati wa utawala wa Mzee Moi, ngome ya Kanu ilikuwa eneo la Bonde la Ufa japo chama hicho pia kilikuwa kikifanya vyema hata katika baadhi ya ngome za upinzani.

Hili lilikuwa dhahiri katika matokeo ya uchaguzi wa 1992 ambao ulikuwa wa kwanza baada ya mfumo wa vyama vingi kukumbatiwa nchini.

Bonde la Ufa lilichangia nusu ya kura ambazo Mzee Moi alipata katika uchaguzi huo uliokuwa na ushindani mkubwa.Katika uchaguzi huo, Mzee Moi alijizolea kura milioni 1.9 huku karibu kura milioni moja zikitoka Bonde la Ufa.

Vivyo hivyo, kwenye kura ya kutetea wadhifa wake 1997, Bw Moi alijizolea asilimia 70 ya kura za bondeni huku mpinzani wake wa karibu Mwai Kibaki akipata asilimia 20 pekee.

Hata hivyo, jinsi ilivyo kwa sasa, Seneta Moi hana ushawishi mkubwa Bondeni akilinganishwa na Naibu Rais William Ruto anayeonekana kuwa kigogo wa siasa za jamii ya Wakalenjin.

Ushawishi

Ni kutokana na ushawishi wa Dkt Ruto ambapo eneo hilo lilimpigia Kinara wa ODM Raila Odinga kura kwa wingi mnamo 2007 kisha Rais Uhuru Kenyatta mnamo 2013 na 2017.

Kwa hivyo, Bw Moi ana mlima mrefu wa kukwea kuhakikisha kuwa Kanu inasalia hai katika Bonde la Ufa kisha maeneo mengine ila kwa sasa itakuwa vigumu kutokana na ushawishi wa Dkt Ruto katika jamii ya Wakalenjin.

Aidha, kumezuka vigogo wa kieneo ambao wana ushawishi katika maeneo yao na kuifanya iwe vigumu sana kwa Kanu kupenya maeneo hayo kama zamani.

Kwa mfano, Kanu enzi hizi ina nafasi finyu sana ya kushinda kiti cha ubunge Nyanza au Pwani kwa kuwa wakazi wengi wanaegemea ODM.

Vivyo hivyo, ilikuwa vigumu kwa chama hicho kushinda viti eneo la Kati au Bondeni mnamo 2017 kutokana na ushawishi wa Jubilee.

Mwanzo wa kupungua kwa umaarufu wa Kanu ulikuwa baada ya uchaguzi 2002 ambapo aliyekuwa Waziri na mwandani wa Mzee Moi, Nicholas Biwott alikihama chama hicho baada ya kushindwa kumbandua Uhuru Kenyatta kama mwenyekiti 2005.

Kabla ya uchaguzi wa 2007, Dkt Ruto alikihama chama hicho na viongozi wengi kisha kujiunga na ODM huku Rais Uhuru Kenyatta pia akibanduka mnamo 2012 na kubuni TNA kisha kuacha chama hicho kigae tu.

Katika uchaguzi mkuu ujao, Kanu inaweza kuongezea idadi ya wabunge wake 10, maseneta wawili na gavana ila kurejelea umaarufu wake wa enzi za utawala wa chama kimoja na miaka ya 90 ni kibarua kigumu.

You can share this post!

Leeds United wakung’uta Watford na kusajili ushindi...

Kafyu: Raia kuumia zaidi vigogo wakieneza corona kijeuri