• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
ONYANGO: Ushauri nasaha ndio dawa ya matatizo ya akili, mauaji

ONYANGO: Ushauri nasaha ndio dawa ya matatizo ya akili, mauaji

Na LEONARD ONYANGO

VISA vingi vya mauaji na watu kujitoa uhai ambavyo vimekuwa vikiripotiwa katika vyombo vya habari hivi karibuni havifai kupuuzwa.

Mauaji hayo yanaogofya na yanaweza kuwa kidokezo tu kuhusu madhara ya janga la virusi vya corona kwa afya ya akili.

Ndani ya mwezi mmoja uliopita, kumeripotiwa visa tele vya watoto kuua au kujaribu kuua wenzao, wazazi wao au walimu. Kadhalika, kumekuwa na ripoti nyingi za watu wazima kuua au kujaribu kutekeleza mauaji huku wengine wakijitoa uhai.

Kisa cha hivi karibuni ni cha afisa wa polisi wa kituo cha Nguruki, Kaunti ya Tharaka Nithi ambaye alhamisi mwili wake ulipatikana ukining’inia katika nyumba ya jirani.

Kwa mujibu wa polisi, afisa huyo wa polisi wa umri wa miaka 35, alijaribu kujikata shingo kabla ya kujinyonga.

Siku hiyo hiyo, wakazi wa mtaa wa Njiru, Kasarani, Kaunti ya Nairobi walipigwa na mshtuko baada ya Margaret Muchemi kuuawa na kisha mwili wake kuteketezwa na mwanaume anayeaminika kuwa mpenzi wake.

Maafisa wa polisi wiki iliyopita, walikamata mwanafunzi wa Kidato cha Nne katika Kaunti ya Bomet kwa madai ya kushambulia mwanafunzi mwenzake wa kike kwa panga.

Mauaji ambayo yamezua gumzo nchini ni yale yaliyotokea mwanzoni mwa mwezi huu, ambapo Nicholas Njoroge, 55, mkewe, watoto wawili na mfanyakazi waliuawa kinyama katika eneo la Kagongo Karura, Kiambaa, Kaunti ya Kiambu.

Mwana wao Lawrence Simon Warunge ni miongoni mwa washukiwa wakuu wa mauaji hayo.

Jumatatu iliyopita, polisi walinasa mwanafunzi wa Kidato cha Tatu kwa madai ya kushambulia na kuua mlinzi wa shule yao katika Kaunti ya Vihiga.

Kulingana na polisi, mwanafunzi huyo alimuua mlinzi alipojaribu kuingilia kati alipokuwa akiwashambulia wanafunzi wenzake.

Wikendi iliyopita, polisi walikamata Christopher Mburu Wakahiu, 26, kwa madai ya kuua ndugu yake kwa kumdunga kisu katika eneo la Murang’a.

Pasta wa zamani Joel Mogaka, alinaswa wiki mbili zilizopita kwa madai ya kuua mkewe na kisha kupeleka mwili wake katika mochari.

Visa hivyo vyote na vingine vingi ni ishara kwamba kuna tatizo ambalo linafaa kushughulikiwa kwa haraka.

Tafiti ambazo zimefanywa katika mataifa mbalimbali zinaonyesha kuwa janga la virusi vya corona limechangia pakubwa katika kuongezeka kwa visa vya matatizo ya akili. Matatizo hayo yanachangiwa na msongo wa mawazo.

Ripoti iliyotolewa hivi karibuni na Shirika la Afya Duniani (WHO), ilionyesha kuwa janga la virusi vya corona limeongeza kwa kiasi kikubwa idadi ya watu wanaohitaji huduma za afya ya akili.

Ripoti hiyo ilionyesha kuwa mataifa mengi ya Afrika, ikiwemo Kenya, hayajachukulia kwa uzito suala la huduma za afya ya akili.

Takwimu za WHO zinaonyesha kuwa watu wanne hujitoa uhai kila siku nchini Kenya kutokana na matatizo ya akili.

Visa vya watu kujitoa uhai na kuangamiza wengine huenda vikaongezeka mwaka huu iwapo serikali haitachukua hatua za haraka kuhamasisha Wakenya kuhusu umuhimu wa kutafuta huduma za ushauri nasaha. Serikali inafaa kuhakikisha kuwa Wakenya wanapata huduma za ushauri nasaha kwa bei nafuu.

You can share this post!

TAHARIRI: Dawa za nguvu za kiume zidhibitiwe

WARUI: Hatua ya dharura yahitajika kuzima utovu wa nidhamu...