• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 6:39 PM
PATA USHAURI WA DKT FLO: Ukuvu mdomoni ni ishara ya HIV?

PATA USHAURI WA DKT FLO: Ukuvu mdomoni ni ishara ya HIV?

Mpendwa Daktari,

Hivi majuzi marafiki zangu waliniambia kwamba mojawapo ya mbinu ya kutambua iwapo mtu ana virusi vya HIV ni kwa kumuangalia mdomoni kuona iwapo ana ukuvu wa mdomoni (oral thrush).

Hiki ni kidokezi tosha cha kutambua iwapo mtu ana virusi hivi, au kuna matatizo mengine ya kiafya yanayosababisha hali hii?

George, Nairobi

Mpendwa George,

Mbinu pekee na ya uhakika kujua hali ya HIV ya mwenzako ni kwa kupimwa. Mtu anapoambukizwa virusi vya HIV anaweza dumu kwa kati ya miaka minane na kumi kabla ya kuanza kuonyesha ishara zozote.Aidha, wale wanaopokea matibabu na viwango vya virusi hivi mwilini viko chini, hawatakumbwa na maambukizi kama ukuvu wa mdomoni. Kumbuka kwamba maradhi yoyote yanayoathiri kingamwili ya mhusika yaweza mfanya mtu kukumbwa na ukuvu wa mdomoni. Hii ni pamoja na HIV, kisukari, maradhi ya figo, matatizo ya kihomoni, kansa, uzee, umri mdogo sana na matumizi ya dawa za kusisimua misuli na za kutibu kansa.

Mpendwa Daktari,

Nina umri wa miaka 37 ambapo mimi ni mama wa watoto watatu. Wawili niliwazaa kupitia upasuaji. Pamoja na mume wangu tumekuwa tukifikiria kupata mtoto mwingine, lakini nakumbuka madaktari walinishauri nisifanyiwe upasuaji wa uzazi kwa mara nyingine. Hatari zipi ambazo huenda nikakumbana nazo ikiwa nitashika mimba tena?

Janet, Nairobi

Mpendwa Janet,

Baada ya kufanyiwa upasuaji mara mbili wakati wa kujifungua, unaweza shika mimba tena mradi usubiri kwa kati ya miezi 18 na 24 baada ya kupata mtoto wa mwisho.

Wakati wa kujifungua, utalazimika kufanya hivyo kupitia upasuaji, shughuli ambayo lazima ipangiwe.

Usijaribu kujifungua kupitia njia ya kawaida kwani kuna hatari ya uterasi kupasuka unapokumbwa na uchungu wa uzazi. Kuna uwezekano kwamba sehemu iliyokatwa wakati wa upasuaji imeacha gofu.

Ikiwa mji utajishikisha katika sehemu hii, huenda ukasababisha matatizo wakati wa ujauzito, japo sio jambo ambalo waweza dhibiti. Kutokana na sababu kuwa tayari una miaka 37, litakuwa jambo la busara ikiwa utashika mimba haraka iwezekanavyo, kutokana na hatari zinazohusishwa na umri mkubwa.

You can share this post!

Mshukiwa wa unajisi aponea kuteketezwa Kambi Moto

SHINA LA UHAI: Hofu ya ongezeko la saratani ya mapafu nchini