• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 9:01 PM
PAUKWA: Madhila ang’amua subira huvuta heri

PAUKWA: Madhila ang’amua subira huvuta heri

MADHILA alifanya kazi ya utwana katika kiambo cha Bwana Kizito.

Uhusiano baina yake na mwajiri wake ulikuwa wa kufana. Bwana Kizito alimlipa mshahara wake kwa wakati unaofaa na kumwongezea marupurupu mengine ili kumtia ari ya kutenda kazi.

Madhila aliingiwa na wazo la kuyaboresha maisha ya aila yake kupitia pesa alizopokea kwa bosi wake.

Alitaka kujenga angalau nyumba ndogo ya bati ili kuihamisha aila yake kutoka kwenye kibanda cha mbavu za mbwa ilimoishi.

Wakati madhila alipokuwa ameanza kujiwekea akiba kwa ajili ya kufanikisha mradi wa ujenzi ndipo nchi yake ilipokumbwa na mabadiliko ya kiuchumi.

Ulizuka zuu ugonjwa wa kutisha usiokuwa na dawa wala kafara. Ugonjwa huo uliathiri sekta mbalimbali za taifa licha ya kuwaangamiza watu.

Biashara za Bwana Kizito katika jiji la Leondani zilipoteza faida kutokana na homa hiyo ambayo iliendelea kuenea kwa kasi kama moto kwenye kichaka kikavu.

Wasemao kuwa mtego wa panya huwanasa waliomo na wasiokumwemo hawakukosea. Punde si punde, kazi ya Madhila pia iliathiriwa.

Hakulipwa mshahara wake mapema ilivyokuwa hapo awali. Marupurupu aliyokuwa ameyazoea nayo yalianza kuadimika kama maziwa ya kuku! Ilikuwa vigumu kwa Madhila kuyakidhi mahitaji ya msingi ya aila yake kwa sababu pesa alizozipata alizitumia kulipia madeni.

Mambo yalikuwa mabaya zaidi, Bwana Kizito alipokoma kabisa kumlipa Madhila mshahara. Kila wakati Madhila alipomkumbusha kuwa hakuwa amemlipa, alimwambia: ‘‘Ninajua wala usijali, nitakulipa tu.’’

HADITHI ITAENDELEA

  • Tags

You can share this post!

Mbappe afunga mabao matatu dhidi ya Metz na kuibuka...

Wazazi kukamatwa kwa kuficha watoto wahalifu

T L