NA ENOCK NYARIKI
GIZA la kaniki lilitanda kote katika shule ya wavulana ya Jitahidi.
Sauti pekee zilizosikika japo kwa aliyepita nje ya mabweni ya wavulana hao, ni mikoromo yao. Walikoroma mfano wa vyura bwawani.
Sauti zao zilipanda na kushuka kana kwamba zilishindana na kuhimizana. Kwenye upembe huu na ule ulisikika mlio mmoja mmoja wa wadudu waitwao chenene. Hawa walitafuta chakula chao lakini kwa tahadhari. Walilia na kunyamaza mithili ya alamu ya saa. Hayo ndiyo maajabu ya ulimwengu hasa. Kilichotaka kula kuogopa kuliwa!
Kwa kawaida saa kama hizo, wanafunzi wa kidato cha nne wangekuwa darasani wakijisomea mpaka saa nne usiku mchanga.
Hata hivyo, kwa kuwa ilikuwa wikendi, wote walienda kulala ili kujiandaa kwa ajili ya ibada ya Jumapili. Taa ya umeme iliyotundikwa kwenye ukuta mrefu wa bweni mojawapo ilitoa mwangaza hafifu ambao haukuyamulika vizuri mabweni mengine.
Hata miti iliyopandwa kuzunguka mabweni hayo ilifanya vivuli dhaifu vilivyofanana na miguu ya mtu mrefu.
Mwalimu Hamisi alinyatanyata na kusimama chini ya ukuta uliozunguka bweni la Luwenzori. Luwenzori ni bweni lililojengwa mashariki ya shule.
Hatua chache kutoka pale aliposimama palikuwa pametengenezwa alama za miguu ya watu.
Kuna uwezekano kwamba kuna baadhi ya wanafunzi waliotumia sehemu ile kuondoka shuleni.
Mchana huo, Mwalimu Hamisi alikuwa amemwita mkuu wa shule na kumwonyesha palipokuwa na alama zile. Sasa aliweka mtego wake ili kuthibitisha wasiwasi aliokuwa nao.
HADITHI ITAENDELEA
Subscribe our newsletter to stay updated