• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 7:55 AM
Serikali ya Mwangi Wa Iria yatamatisha utoaji wa kilo 700,000 za mbegu za mahindi

Serikali ya Mwangi Wa Iria yatamatisha utoaji wa kilo 700,000 za mbegu za mahindi

Na MWANGI MUIRURI

MSAFARA wa upeanaji mbegu za mahindi kwa wakulima wa Kaunti ya Murang’a hatimaye ulitamatishia shughuli hiyo kaunti ndogo ya Kigumo Jumanne jioni ambapo wakulima wa eneo hilo walipokezwa kilo 60,000.

Serikali ya Gavana Mwangi wa Iria tangu 2015 imekuwa ikitoa mbegu hizo pamoja na fatalaiza ya bure kwa wakulima hao ikilenga kuwahami na uwezo wa utoshelevu wa chakula na pia ziada ya mavuno ya kushirikishwa biashara.

Mpango huu wa sasa ulizinduliwa Ijumaa iliyopita katika maadhimisho ya sherehe ya Pasaka na ambapo ukitamatishwa, ulikuwa umetoa kilo 700,000 kwa wakulima 350,000 kila mmoja akipata kilo mbili za mbegu hizo.

Waziri wa Kilimo wa Kaunti hiyo Bw Albert Mwaniki ndiye alikuwa kinara wa msafara huo.

“Tumekuwa tukisambaza mbegu hizo kila mwaka tangu 2015 na nia yetu ni kuwahami wakulima na uwezo wa kukumbatia mbegu zilizoidhinishwa kuwa salama, faafu na zilizo na uwezo wa kuimarisha mavuno,” akasema Bw Mwaniki katika Kaunti ndogo ya Kandara.

Alisema kuwa mbegu hizo ziko na uwezo wa Kutoa Kati ya magunia 25 na 30 kwa kila ekari akisema kuwa kwa siku zijazo Serikali hiyo itakuwa ikitoa fatalaiza na mbolea ya mifugo ili kuimarisha uwezo wa mbegu hizo kuafikia kilele cha mavuno.

Bw Mwaniki alisema ushirikiano wa serikali kuu na ile ya Kaunti utaishia kuafikia mpango wa kusambaza maji ya kilimo cha unyunyiziaji, hali ambayo itaishia kuipa Kaunti uwezo wa kujilisha na pia kuwa na cha ziada cha kushirikisha biashara.

Kwa sasa, Kaunti ya Murang’a na pia ukanda wa Mlima Kenya unajiandaa kupokea mvua ya msimu wa Kati ya Aprili na Agosti.

Serikali kuu tayari imetoa tahadhari kuwa takriban Wakenya 1.5 milioni wako katika hatari ya kukumbwa na makali ya njaa kufikia Agosti.

Bw Mwaniki alisema kuwa Kaunti ya Murang’a imepata hakikisho kuwa itapata mvua ya kutosha bora tu kuwe na matumizi ya mbegu mwafaka zinazoambatana na hali ya kimazingira na pia fatalaiza zinazofaa na kwa wakati ufaao.

  • Tags

You can share this post!

Jinsi Taa Steriliser inavyoweza kufanya pesa, vifaatiba na...

Diwani ndani miaka minane kwa kujaribu kuokoa watu...