• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 7:55 AM
Shirika la kutafutia wakulima soko lawahimiza kukuza mimea inayostahimili athari za mabadiliko ya tabianchi

Shirika la kutafutia wakulima soko lawahimiza kukuza mimea inayostahimili athari za mabadiliko ya tabianchi

Na SAMMY WAWERU

SHIRIKA moja la kutafutia wakulima soko la mazao yao nje ya Bara Afrika limewahimiza kukumbatia ukuzaji wa mimea inayostahimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

Janga la ukame, mkurupuko wa magonjwa na wadudu ni miongoni mwa athari zinazojiri kutokana na mabadiliko ya tabianchi.

Shirika la Fairtrade Africa (FTA) limesema wakulima wakikuza mimea yenye ustahimilivu wa hali ya juu kwa athari hizo, mataifa yanayohangaishwa na kero ya baa la njaa yatakuwa na usalama wa chakula.

“Tunahimiza wakulima wafanye utafiti na kutambua mimea inayoweza kustahimili makali ya athari za mabadiliko ya tabianchi,” akashauri Bw Chris Oluoch, Mkurugenzi wa Mikakati FTA, katika hafla iliyoandaliwa jijini Nairobi na kuleta pamoja kampuni na mashirika ya yanayochangia uzalishaji wa chakula, maua na pamba nchini.

Kwenye mahojiano, afisa huyo aliambia Taifa Leo kwamba shirika hilo limeweka mikakati kabambe kuona wakulima na mashirika wanachama wake, wanakabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

“Tumeweka mipango na sheria kuona wanaboresha shughuli za kilimo,” akasema.

“Isitoshe, tunawapiga jeki waweze kukumbatia vigezo vya kilimo bora, katika mchakato mzima kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi,” Bw Oluoch akaelezea.

Mabadiliko ya tabianchi yamesababisha hali ya anga kubadilika kwa kiasi kikubwa, kaunti zinazoshuhudia kiangazi mara kwa mara nchini (ASAL), zikiendelea kuhangaishwa na ukame na njaa.

Kaunti zipatazo 24 zina mamilioni ya wakazi ambao serikali isipotafuta suluhu ya kudumu dhidi ya ukame, huenda wakafa njaa.

You can share this post!

Brazil yaita kambini masogora wanane wanaopiga soka...

Bobi Wine azimwa kuelekea Amerika kwa kutotimiza masharti...