• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Sonko awaka moto, akijigamba na hela kama njugu

Sonko awaka moto, akijigamba na hela kama njugu

NA SAMMY WAWERU 

ALIYEKUWA Gavana wa Nairobi Mike Sonko amegeuka kuwa gumzo la mitandao, kufuatia ufichuzi wa michuzi ya hela anazomiliki. 

Jumanne, Mei 16, 2023 safu za mitandao ya kijamii na hata vyombo vya habari viligaragaza mjadala huo moto wa majigambo.

Hii ni baada ya gavana huyo wa kitambo Mei 15, 2023 kutoa video inayoonyesha akimiminia sifa utajiri wake.

“…Pesa za kuharibu na bibi zangu…” Bw Sonko alidai.

Kupitia kanda hiyo ya dakika 2 na sekunde 50, Sonko anaskika akichemka kama maji moto chunguni, kilichoinjikwa jikoni.

Ni kana kwamba kuna aliyemkosea akimshusha hadhi kifedha, kwa mujibu wa maneno aliyotumia mengine tusiyoweza kuchapisha kwa sababu ni ya aibu.

Hadi kufikia sasa, haijulikana aliyekwaza mwanasiasa huyo mwenye ushawishi mkubwa mitandaoni.

“Ati sina pesa…Hizi ni pesa za ziada za mafuta ya gari,” alielezea akifungua mojawapo ya masanduku mawili yaliyokuwa na mabunda ya noti.

Aidha, zilikuwa noti za Dola na pesa za Kenya akisema masunduku aliyonasa kupitia video yana mamilioni.

Bw Sonko anajulikana kwa kusaidia wasiojiweza katika jamii, hasa visa vya wanaoangaziwa mitandaoni na vyombo vya habari.

Ana baadhi ya watoto anaosaidia wanaotoka familia maskini, na wengine mayatima.

Desemba 2020, madiwani (MCA) Kaunti ya Nairobi walimvua taji la ugavana, maamuzi ya serikali ya kaunti yakitiwa muhuri na bunge la seneti.

Aliondolewa ofisini kwa tuhuma za matumizi mabaya ya ofisi, ufujaji wa raslimali ya umma na ufisadi.

Aliyekuwa naibu wake, Bi Ann Kananu alimrithi.

Mwaka 2022, jaribio lake kuwania kiti cha ugavana Mombasa hata hivyo halikufua dafu kufuatia kung’atuliwa kwake 2020.

 

 

 

  • Tags

You can share this post!

Sakata ya neti za kuzuia mbu yauma wakuu wa Kemsa

Raia kuendelea kuumia zaidi

T L