• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 10:55 AM
TAHARIRI: Kikosi maalumu kitumwe Laikipia

TAHARIRI: Kikosi maalumu kitumwe Laikipia

KITENGO CHA UHARIRI

UFICHUZI kwamba majangili wanaohangaisha wakazi wa Kaunti ya Laikipia wanatumia bunduki za maangamizi makubwa kuliko zile zinazotumiwa na polisi, unahofisha.

Kulingana na Kamishna wa Bonde la Ufa, Bw George Natembeya, majangili hao wanatumia bunduki za M16 ambazo kwa kawaida hutumiwa na majeshi ya kigeni ambayo yamekuwa yakifanyia mafunzo katika Kaunti ya Laikipia.

Bw Natembeya pia alifichua kwamba serikali haina ufahamu kuhusu mahali majangili hao walikopata silaha hizo hatari.

Kwa upande mwingine, maafisa wa humu nchini wanatumia bunduki aina ya AK47 na G3 hivyo kuwa vigumu kuwamaliza majangili hao.

Watu wasiopungua 12 wameuawa na zaidi ya nyumba 50 kuteketezwa kufikia jana katika eneo hilo. Kwa mujibu wa ripoti, shule zisizopungua sita zimefungwa kufuatia machafuko hayo.

Inaogofya kwamba majangili hao wamekuwa wakitekeleza mashambulio usiku dhidi ya raia licha ya kuwepo kwa vikosi mbalimbali vya usalama kama vile maafisa wa kupambana na wizi wa mifugo (ASTU) na GSU.

Mnamo Julai 28, 2021, waziri wa Usalama, Dkt Fred Matiang’i alipozuru Kaunti ya Laikipia alitoa onyo kali dhidi ya majangili na kutoa makataa ya siku saba kwa wafugaji waliokuwa wakichunga mifugo yao katika mashamba ya kibinafsi, kuondoka.

Lakini makataa hayo ya Waziri Matiang’i hayakuwa na athari yoyote kwani majangili hao wangali wanaendelea kuhangaisha wakazi.

Kulingana na Katibu wa wizara ya Usalama, Dkt Karanja Kibicho, suala la usalama katika Kaunti ya Laikipia limeingizwa siasa – hali ambayo imetatiza juhudi za kudhibiti majangili.

Jambo la kushtua zaidi ni kwamba majangili hao wamekuwa wakijitokeza tu kila mara uchaguzi unapokaribia tangu 1992.

Suala la ukosefu wa usalama katika Kaunti ya Laikipia limegeuka donda ndugu sawa na eneo la Kapedo (mpakani mwa Kaunti za Baringo na Turkana) ambapo serikali imeshindwa kudhibiti majangili ambao wamekuwa wakihangaisha watu kwa miaka na mikaka.

Serikali haina budi kuchukua hatua kali kwa kuzindua kikosi maalumu cha kukabiliana na majangili hao katika eneo la Laikipia sawa na ilivyofanya 2008 dhidi ya wanamgambo wa Sabaot Land Defence Force (SLDF) katika eneo la Mlima Elgon kupitia ‘Operation Okoa Maisha’.

You can share this post!

Cheruiyot tayari kuonyesha bingwa wa Olimpiki Ingebrigtsen...

Mifuko yatumika kama ushahidi wa mauaji ya wakili Kimani...