• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 PM
TAHARIRI: Serikali ikabili baa la njaa mapema

TAHARIRI: Serikali ikabili baa la njaa mapema

KITENGO CHA UHARIRI

RIPOTI kwamba janga la njaa tayari limeanza kukatiza maisha ya Wakenya kaunti 12 zikiathirika, ni suala la kuhofisha na linalofaa kuchukuliwa kwa uzito na viongozi nchini.

Vile vile hatua za dharura zinafaa kutekelezwa kwa haraka.

Kwa kawaida, kila mara zinapochipuka taarifa kuhusu vifo kutokana na njaa, serikali hukimbia kuzipinga huku ikijiondolea lawama.

Aidha hakuna takwimu kuhusiana na idadi ya waliofariki au kuathirika na njaa.

Si ajabu wakati mwingine maafisa wa serikali hutoa taarifa ya jinsi walivyo tayari kupambana na baa la njaa ilhali kwa hakika huwa ni siasa na ahadi tupu za kuwafunga wananchi macho.

Maisha ya Mkenya mmoja yanapopotezwa yana thamani kubwa kiasi kwamba kila mbinu inafaa kutumiwa kuyalinda.

Hii ni kwa sababu yanapotoweka, hakuna njia hata moja inayoweza kutumika kuyarerejesha tena upya.

Wakati mwingine serikali huwa inasubiri hadi pale watu kadhaa wanafariki na janga la njaa kukithiri ndipo ianze kuchukua hatua za kuokoa raia wake.

Utaona serikali ikitegemea mashirika yasiyo ya serikali kama Red Cross, World Vision kuwafaa waathiriwa huku ikiwatazama tu!

Miaka ya hapo nyuma Wakenya walionekana kuungana pamoja kuchangia wenzao ili kuwanusuru kutokana na makali ya njaa.

Tayari vifo kutokana na njaa na ukosefu wa maji vimeripotiwa katika Kaunti ya Samburu. Hali ya ukame imetajwa maeneo ya Kaskazini Mashariki, Pwani na Mashariki mwa Kenya.

Maeneo mengine ni Turkana, Baringo na Bonde la Ufa kwa ujumla ambapo wanyama wa mifugo kadhaa wamefariki kutokana na kiangazi kikali. Si siri kwamba mifugo ndio asili ya mlo na tegemeo la kifedha la wafugaji nchini.

Ni haki ya Wakenya kupewa hakikisho la usalama wa chakula. Pia ni haki ya kila Mkenya kupata maji safi.

Kwa upande mwingine ni jukumu la serikali kulinda raia wake dhidi ya njaa. Vivyo hivyo inafaa kutoa maji safi kwa wananchi bila kushurutishwa.

Kutokana na miradi duni iliyoanzishwa na serikali kuu, zikiwepo zile za kaunti, baadhi ya Wakenya wamejipata katika hali ya kusononeka kwa madhara ambayo hawajui asili wa fasili yake.

Mingi ya miradi ya mabwawa nchini ilizinduliwa miaka kadha iliyopita na fedha nyingi kuwekezwa humo lakini matokeo yake yamekuwa ya kusikitisha. Badala ya miradi hii kukamilishwa na kufaidi wakazi, hatimaye husambaratika na mamilioni kuishia katika mifuko ya watu binafsi kwa misingi ya ufisadi.

Miradi mingine ya unyunyiziaji maji mashamba nchini ilipitia mkondo huo huo na kuacha raia na matumani hewa.Serikali ziungane mara moja kuokoa maisha ya Wakenya kutokana na makali ya njaa sasa hivi.

Mikakati ya kukomesha janga hili kabisa ifufuliwe na kukelezwa. Taifa linaloheshimiwa ni lili linalowajali raia wake hasa kuwatosheleza mahitaji ya kimsingi ikiwepo hitaji la chakula.

You can share this post!

DNA yaonyesha mjukuu wa Moi ndiye baba ya watoto anaopinga...

Kingi apuuzilia mbali shinikizo kumtaka ajiunge na Ruto