• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
TAHARIRI: Serikali isilazimishe walimu kusoma tena

TAHARIRI: Serikali isilazimishe walimu kusoma tena

NA MHARIRI

WAKUU wa vyama vya kutetea walimu nchini ni wasaliti kwa kukubali kuingia katika mkataba ya kuwataka walimu waongezee masomo yao kila baada ya miaka mitano na kujigharimia fedha zinazohitajika kufaulisha mpango huo.

Chama cha Walimu wa Shule ya Upili na Vyuo Anuwai (Kuppet) na kile cha Knut, vimewasaliti walimu kwa kuwa mkataba huo unasema walimu wenyewe watajilipia karo.

Pia Tume ya Kuwaajiri Walimu ambayo iliingia katika maelewano hayo na Knut ilipendekeza kuwa leseni au nambari ya TSC itarefushwa kila baada ya miaka mitano baada ya kila mwalimu kukumbatia masomo hayo. Si vibaya kwa kila mwalimu kujiongezea elimu ambayo ni hazina isiyokwisha.

Kila mtu anafaa kujifahamisha mambo mapya wala si kusubiri hadi miaka mitano pekee.Hata hivyo, Knut na Kuppet zinaonekana kama vyama visivyozingatia maslahi ya walimu tena.

Kwa kuingia mkataba huo, vyama hivyo havikuzingatia kuwa walimu wanafamilia na majukumu mengine ya kimsingi ambayo yanawahitaji kuwajibikia kifedha.

Je, mwalimu ambaye atakuwa na watoto wake shule au vyuoni ataweza kugharimia karo yao kivipi iwapo wakati huo yeye pia atakuwa akitakiwa awe shuleni kwa gharama yake mwenyewe?

Walimu hawajaongezwa mshahara wowote. Hata makubaliano ya mwaajiri wao pamoja na vyama hivyo ya nyongeza ya mishahara bado hayajatekelezwa. Itakuwa vigumu kupata pesa za masomo hayo ikizingatiwa kuwa wengi wao pia huwa wana mikopo mikubwa ya kulipa kila mwezi.

Taaluma ya ualimu vyuoni huchukua miaka minne au miwili kuisomea. Je, ina maana kuwa muda huu wote utakuwa umepotea iwapo mwalimu hatajisajili katika masomo haya mapya na leseni yake kutorefushwa ?Pia kumekuwa na malalamishi kuwa mkataba huu haukuwashirikisha walimu kupitia matawi ya vyama vyao.

Kwa hivyo, kuna uwezekano TSC na Kuppet na Knut zilipuuza hitaji la ushirikishaji walimu kuhusu suala hili linalowaathiri.

Walimu walifaa kusikizwa na maoni yao kutiliwa manani. Ni vyema iwapo TSC na uongozi wa vyama hivi uwazie upya mpango huu wa masomo na kutumia mbinu ambayo itakubalika na walimu. Viongozi wa Knut na Kuppet nao wamefeli na wanaonekana kutokuwa na ari ya kutetea walimu dhidi ya serikali.

You can share this post!

Abiria kutumia reli kutoka Mombasa hadi Malaba kuanzia...

Nacada yalilia kituo cha kurekebisha tabia