JUMA hili naomba tuangazie swali lifuatalo katika Tamthilia ya Kigogo.
Ami? Tangu lini ukawa ami yangu?
(a) Eleza muktadha wa dondoo. (alama 2)
(b) Taja mbinu iliyotumika katika dondoo hili. (alama 2)
(c) Eleza sifa za msemaji (alama 2)
(d) Bainisha maudhui ya nafasi ya mwanamke ukizingatia mhusika huyu. (alama 4)
(a) Maneno haya yanasemwa na Tunu akiwa ofisini mwa Majoka, akimjibu Majoka baada ya kumtaka amsalimu yeye ‘ami’ yake.
(b) Swali balagha – Ami? Tangu lini ukawa ami yangu?
(c) Mwenye msimamo dhabiti – Tunu ameamua kuwa hatakubali kuolewa na Ngao Junior na anashikilia msimamo huo. Mtetezi wa haki – Tunu anashirikiana na wananchi wengine ili kuhakikisha kuwa soko limefunguliwa. Mwenye maono thabiti – Hata baada ya kulemazwa, anaendelea na harakati za ukombozi.
(d) Kwanza, amedhihirisha kuwa, wanawake ni watu ambao wanaweza kusimama kidete ili kutetea maslahi ya wanajamii kwa jumla. Aidha, amedhihirisha kuwa wanawake pia wanaweza kuwania nafasi za uongozi na kuwaongoza watu kikamilifu bila uoga na kwa ujasiri.
Hali kadhalika, kupitia kwa Tunu tumeona kuwa wanawake si watu wa kutamaushwa na waume.
Vilevile amebainisha kuwa,japo wanawake wanahusika katika siasa, bado hawatayasahau majukumu yao ya kike. Aidha, hawatapotoka kimaadili. Anakuwa mshirika wa karibu wa Sudi lakini hajihusishi naye kimapenzi.
Simon Ngige
Alliance High School