JANA Jumatano, Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i, alitangaza kuwa wahudumu wa bodaboda watasajiliwa upya katika vituo 52 vya Huduma Centre kote nchini, kama hatua ya kuondoa wahalifu katika sekta hiyo.
Hii ni baada ya baadhi ya wahudumu wa bodaboda kumshambulia na kumdhulumu mwendesha gari mmoja wa kike, katika barabara ya Wangari Maathai (zamani Forest Road) jijini Nairobi, Ijumaa wiki jana.
Kufuatia tukio hilo Rais Uhuru Kenyatta aliwaamuru maafisa wa usalama waendeshe msako mkali kuwanasa wanabodaboda wakaidi kote nchini.
Lakini kile Rais Kenyatta na waziri Matiang’i wasije wakahau ni kuwa mnamo Aprili 21, 2018 serikali hii hii ilibuni jopokazi kuchunguza changamoto zinazokumba sekta ya bodaboda kwa lengo la kutoa mapendekezo ya kuilainisha.
Lakini karibu miaka minne baada ya jopokazi hili kuwasilisha ripoti yake kwa Waziri Matiang’i na mwenzake wa Uchukuzi James Macharia, mapendekezo yake hayajatekelezwa.
Baadhi ya mapendezo ya jopokazi hilo, ni kwamba wahudumu wote wa bodaboda nchini wasajiliwe rasmi na wapewe vitambulisho maalum vya kidijitali ili kuwaondoa wahalifu katika sekta hiyo.