NA MHARIRI
INASIKITISHA kuwa tangu Desemba 2022, serikali ya Kenya Kwanza haijatuma mgao wa kaunti kwa magatuzi hayo.
Hali hiyo imesababisha mkwamo wa maendeleo katika kaunti zote 47. Pesa hizo hufaa kutumwa kwa awamu nne kwa mwaka, yaani kila baada ya miezi mitatu. Kutokana na ukosefu wa pesa, kaunti hazijawalipa mishahara wafanyakazi kwa miezi minne sasa. Wafanyakazi hao sasa wanaishi kwa neema ya Mungu tu.
Hawawezi kumudu kodi ya nyumba, kulipia watoto wao karo na hata matumizi ya kila siku kama vile chakula na usafiri. Kaunti hizo haziwezi kulipa madeni wala kuzindua miradi mipya ya maendeleo.
Baadhi ya kaunti zimeamua kukopa kwenye benki ili kuendesha shughuli za kimsingi za kaunti. Hii ina maana kuwa zitakapopokea mgao huo, zitalazimika kulipa mikopo hiyo na riba; hii ni hasara inayoweza kuepukwa. Tukio hili pamoja na Serikali ya Rais William Ruto kutaja kwamba haitaweza kuzipa serikali za kaunti Sh407 bilioni inavyostahili, inadhihirisha taswira kuwa yakini utawala wa Kenya Kwanza hauna haja ya kustawisha ugatuzi.
Majuzi Serikali Kuu iliahidi kuzipa serikali za kaunti mgao wa Sh380 bilioni katika mwaka ujao wa kifedha unaoanza Julai 2023, ilhali kisheria zinafaa zipewe Sh407 bilioni kama ilivyoelekezwa na Tume ya Ugavi wa Mapato (CRA). Katiba ya Kenya ya 2010 inaamuru serikali kuu izitengee serikali za ugatuzi angaa asilimia 15 ya jumla ya mapato kulingana na bajeti ya mwaka uliotangulia. Ikizingatiwa kuwa bajeti ya mwaka wa 2021/22 ilikuwa Sh3 trilioni, serikali kuu inastahili kuyapa maeneo gatuzi Sh407 bilioni.
Vilevile, wakati wa kampeni za uchaguzi uliopita, mrengo wa Kenya Kwanza chini ya Rais Ruto, wakati huo akiwa naibu rais, ulisema kwamba hauhitaji mabadiliko ya katiba (BBI) ili kuzipa kaunti mgao wa hadi asilimia 35. BBI ilinuia kuhakikisha katiba inaweka asilimia 35 kama mgao wa chini zaidi wa kaunti. Dkt Ruto, ambaye kwa upande wake alikuwa anapinga marekebisho ya katiba, alisema serikali ingeweza kutoa asilimia hiyo 35 bila kubadilisha katiba kwa kuwa katiba ya sasa inasema kiwango cha chini kiwe asilimia 15 na juu kiwe 35, kwa hivyo, yeyote ambaye angeshinda urais, angeweza kuzipa kaunti zaidi ya asilimia hiyo 15.
Lakini inashangaza kuwa Dkt Ruto sasa hayuko tayari kuzipa kaunti hata hiyo asilimia 15 inayopendekezwa. Serikali yafaa ifuate katiba katika kusuluhisha mgogoro huu mbali na kuharakisha kutoa mgao wa kaunti ili shughuli za ustawi zianze. Bila kujali sababu inayolazimu serikali kuu kuchelewa kutoa mgao wa kaunti, ni muhimu ifanye kila juhudi kunusuru kaunti kama ishara ya nia njema kuhusu makuzi ya mfumo wa ugatuzi nchini.