MNAMO 2008 serikali ya Kenya ilianzisha mradi wa ujenzi wa jiji la kiteknolojia katika eneo la Konza, kwenye mpaka wa kaunti za Machakos na Makueni.
Mradi huo, maarufu kama, ‘Konza Technopolis City’, ulitarajiwa kuvutia wawekezaji katika fani mbalimbali za taaluma ya teknolojia ya habari na mawasiliano (ICT) ambao wangezalisha nafasi za ajira kando na kupiga jeki maendeleo nchini.
Lakini miaka 13 baadaye, utekelezaji wa mradi huo ungali katika awamu yake ya kwanza.
Hii ni licha ya kwamba mradi huo hutengewa mabilioni ya fedha katika bajeti ya kitaifa kila mwaka.
Rais Uhuru Kenyatta anapoondoka afisini baada ya uchaguzi mkuu wa Agosti 9, asije akasahau serikali yake iliahidi kukamilisha mradi huu ambao ilirithi kutoka kwa mtangulizi wake, Mwai Kibaki.