NA WANDERI KAMAU
DHANA inayoendelezwa na baadhi ya viongozi wa mrengo wa Kenya Kwanza kuwasiri wenzao katika muungano wa Azimio la Umoja kama maadui wa nchi haifai kuruhusiwa kujidhihirisha hata kidogo.
Mrengo wa Azimio ni mojawapo ya mirengo mikuu ya kisiasa nchini. Waanzilishi wake wakuu – Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta, Bw Raila Odinga, Bw Kalonzo Musyoka na Bi Martha Karua – ni Wakenya.
Si maadui wa nchi. Si wasaliti wa raia. Hawakufanya kosa lolote kubuni muungano huo, bali ilikuwa haki yao kikatiba kubuni njia ambayo wangetumia kutwaa uongozi nchini.
Mbona baadhi ya viongozi, hasa Naibu Rais Rigathi Gachagua, wanaendelea kuwasawiri watu waliounga mkono muungano huo kama wasaliti wa nchi?
Fikra hii inatokana na malalamishi ambayo yameibuliwa na baadhi ya machifu katika eneo la Mathira, Kaunti ya Nyeri, wanaolalamika kuwa Bw Gachagua anatishia kuwaadhibu kwa kuunga mkono mrengo wa Azimio kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Agosti 9, 2022.
Machifu hao wanadai kuwa mapema wiki hii, Bw Gachagua aliwapigia simu akitishia kuhakikisha wamefutwa kazi.
Bila shaka, huu si mwelekeo mzuri hata kidogo wa kisiasa. Ni hali inayomsawiri Bw Gachagua kama kiongozi mwenye kisasi, na asiyejua tofauti za kibinafsi na kisiasa.
Halikuwa kosa lolote machifu hao – ama Mkenya yeyote yule – kuunga mkono Azimio, kwani ni haki yao kikatiba kufanya hivyo.
Walio katika Azimio si maadui, bali ni Wakenya pia waliolenga kutafuta uongozi japo wakafeli. Mbona wasawiriwe kama maadui?
Subscribe our newsletter to stay updated