• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 11:53 AM
Akida arefusha mkataba wake na PAOK ya Uturuki

Akida arefusha mkataba wake na PAOK ya Uturuki

NA JOHN KIMWERE

MWANASOKA wa kimataifa wa kike Mkenya, Esse Akida amerefusha mkataba wake na klabu ya PAOK Thessaloniki, nchini Uturuki kuichezea kwa muhula mwingine mmoja.

Mchana nyavu huyo wa Harambee Starlets ameongezewa mkataba huo baada ya kucheka na wavu mara 18 na kusaidia klabu hiyo kuhifadhi taji la Ligi Kuu nchini humo bila kupoteza mchezo wowote.

Taarifa ya klabu hiyo iliyochapishwa kwenye tovuti yake ilisema kuwa mchezaji huyo aliibuka mfungaji bora wa kikosi hicho kinachojivunia kubeba ubingwa huo mara 17.

Mpiga gozi akiwa nyumbani Kenya alikuwa akichezea Thika Queens.

Alielezea furaha yake baada ya kutia wino kusakatia kikosi hicho kwa muhula mwingine.

“Bila shaka nimejaa furaha tele kupata nafasi kuendelea kuwa mwana familia wa PAOK. Ninashukuru rais wa PAOK na kocha wake, Athanasios Katsaris na Lefteris Kanata mtawalia kwa kuniaminia na kufikia uamuzi wa kuniongezea muda mwingine kuwa mchezaji wao,” alisema na kuongeza kuwa anatarajia kuendeleza mchezo mzuri na ikiwezekana kufana zaidi kuliko muhula uliopita.

Mwanzo wa ngoma nchini humo mchezaji huyo alijiunga na klabu ya Besiktas.

Mrembo huyo alidokeza kuwa tangu aanze kushiriki soka nchini humo amekuwa rafiki mkubwa na viongozi pia wafuasi wa klabu hiyo.

Aidha alikariri kuwa licha ya kupata jeraha katikati mwa msimu huo anashukuru Mola maana alifanikiwa kutikisa wavu mara 18 na kusaidia klabu hiyo kuhifadhi ubingwa wa ligi kuu.

  • Tags

You can share this post!

Ombi Wajackoyah azimwe kuwania urais kwa sababu ni hatari...

Vipusa wa Ufaransa wakomoa Italia na kuwapa onyo wapinzani...

T L