Na MASHIRIKA
KIPA Emiliano Martinez wa Aston Villa aligeuka tegemeo kubwa la Argentina waliowacharaza Uruguay 1-0 katika mchuano wao wa pili wa Copa America katika Kundi A mnamo Ijumaa usiku.
Bao la pekee na la ushindi katika mechi hiyo lilifumwa wavuni na Guido Rodriguez baada ya kushirikiana na nyota Lionel Messi katika dakika ya 13.
Argentina walishuka dimbani kwa ajili ya gozi hilo wakitawaliwa na kiu ya kusajili ushindi baada ya kuambulia sare ya 1-1 dhidi ya majirani zao Chile mnamo Juni 15, 2021.
Argentina kwa sasa wanajivunia alama nne sawa na Chile ambao pia walisajili ushindi wa 1-0 dhidi ya Bolivia katika mchuano wao wa Ijumaa usiku kwenye Kundi A.
Chini ya kocha Lionel Scaloni, Argentina watapepetana na Paraguay katika mechi ijayo mnamo Juni 22 kabla ya kufunga kampeni za Kundi A dhidi ya Bolivia mnamo Juni 29. Paraguay wanashikilia nafasi ya tatu kundini kwa pointi tatu huku Uruguay na Bolivia wakivuta mkia bila alama yoyote kibindoni.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO