• Nairobi
  • Last Updated May 9th, 2024 1:42 PM
Kinda Caleb Atuta ajisuka akilenga kufikia viwango vya CR7

Kinda Caleb Atuta ajisuka akilenga kufikia viwango vya CR7

Na PATRICK KILAVUKA

LICHA ya kinda Caleb Atuta kuwa na umri wa miaka tisa pekee, anadhihirisha kwamba uwezo kwa kukuza kipaji umo katika ari ya mchezaji mwenyewe kujibidiisha mithili ya mchwa kuwasha mshumaa wa talanta yake.

Mwanasoka Atuta anacheza safu ya kiungo mvamizi. Ana chenga maridhawa, hutamba na boli na hufunga mabao kwa ustadi.

Anaamini kwamba kupiga zoezi ni hatua ambayo inamwelekeza katika barabara ya kufaulu kukuza kipawa ambacho kitakuwa cha kumfaa maishani. Isitoshe, juhudi hulipa

Mwanasoka huyu ni mwana wa Jared Omboko na Rhoda Omboko.

Alianza kusakata boli akiwa darasa la pili Shule ya Msingi ya Kangemi.

Alijiunga na timu ya Zion Winners baada ya pitapita za kocha wake Charles Wentindi ambaye ni mchezaji wa timu ya Zion Winners Senior zilikuwa za jicho pevu kwake.

Kinda chipukizi wa soka Caleb Atuta akifanya zoezi akiwa na kocha wake Charles Wentindi uwanjani Kihumbuini. PICHA | PATRICK KILAVUKA

“Nilikuwa na muona akicheza kwa weledi kwenye ploti. Nilijaribu kumualika kwenye uwanja kuhudhuria mazoezi na alifanya mambo kweli kwenye zoezi na akasajiliwa katika kikosi cha wasiozidi miaka kumi na moja kabla kumjumuisha katika kikosi cha miaka ya kumi na mitatu.

Ni mchezaji ambaye pia ana nidhamu ya juu na akiendelea hivyo atakuwa mwanasoka wa kutegemewa sana,” alieleza kocha wentindi ambaye anamlea kipaji.

Kwa sasa anasakatia timu hiyo katika Ligi ya Chama ya Soka Nairobi Kaunti (NCFA) cha wasiozidi miaka 13 ambapo kufikia sasa amefunga mabao nne.

Yeye hudhuria mazoezi na kucheza mechi za ligi uwanjani Kihumbuini wikendi.

Ingawa changamoto yake ni jezi, buti na gwanda la kulivalia kwa miguu, anasema mzazi wake anajaribu kumnunulia hali ambayo inampa motisha zaidi ya kukuza talanta yake.

“Ananisaidia kwa vyo vyote vile kuhakikisha ninaendeleza upigaji shughuli za kabumbu,” alikariri mwanasoka huyo.

Timu ambazo anazipenda hapa nchini ni ya mtaani ya Matrix FC na Gor Mahia mbali na kuwa shabiki wa Manchester United ughaibuini ambapo anafurahia mchezaji Cristiano Ronaldo.

You can share this post!

Mshukiwa wa ujambazi auawa kwa kupigwa risasi na polisi...

Arsenal wakomoa West Ham United na kuingia nne-bora EPL

T L