Na MASHIRIKA
PIERRE-Emerick Aubameyang alifungua akaunti ya mabao kambini mwa Barcelona kwa kujaza kimiani magoli matatu katika ushindi wa 4-1 uliosajiliwa na miamba hao dhidi ya Valencia katika Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) mnamo Jumapili.
Ushindi huo uliendeleza rekodi ya kutopigwa kwa Barcelona katika mechi tisa zilizopita ligini tangu Disemba 4, 2021.
Aubameyang aliyesajiliwa na Barcelona kutoka Arsenal mwishoni mwa Januari 2022, alifungulia waajiri wake karamu ya mabao katika dakika ya 23 kabla ya kufunga magoli mengine katika dakika za 38 na 63. Mechi hiyo ilikuwa yake ya kwanza ndani ya jezi za Barcelona.
Mabao mengine ya Barcelona yalifungwa kupitia Frenkie de Jong na Pedri Lopez baada ya Carlos Soler kurejesha Valencia mchezoni. Aubameyang, 32, angalifunga mabao zaidi mwishoni mwa kipindi cha pili ila akazidiwa ujanja na kipa Giorgi Mamardashvili.
Barcelona kwa sasa wanakamata nafasi ya nne jedwalini kwa alama 42, nne nyuma ya Real Betis ambao wametandaza mchuano mmoja zaidi.
Sevilla wanashikilia nafasi ya pili kwa pointi 51, sita nyuma ya viongozi Real Madrid. Valencia ambao wamepiga jumla ya mechi saba zilizopita ligini bila ya kushinda yoyote, wanakamata nafasi ya 12 kwa pointi 30.
Matokeo ya La Liga (Jumapili):
Valencia 1-4 Barcelona
Espanyol 1-1 Sevilla
Real Betis 2-1 Mallorca
Bilbao 4-0 Real Sociedad
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO