• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 7:02 PM
Chelsea wakomoa Lille na kutia guu moja ndani ya robo-fainali za UEFA

Chelsea wakomoa Lille na kutia guu moja ndani ya robo-fainali za UEFA

Na MASHIRIKA

CHELSEA walitia guu moja ndani ya robo-fainali za Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) baada ya kutandika Lille 2-0 katika mchuano wa mkondo wa kwanza wa hatua 16-bora mnamo Jumanne usiku ugani Stamford Bridge.

Kai Havertz aliwaweka Chelsea kifua mbele baada ya kushirikiana na Hakim Ziyech katika dakika ya nane. Christian Pulisic alipachika wavuni bao la pili la waajiri wake baada ya kukamilisha krosi kutoka kwa N’Golo Kante katika dakika ya 63.

Fowadi Romelu Lukaku ambaye makali yake yameshuka pakubwa kambini mwa Chelsea aliletwa uwanjani katika kipindi cha pili. Hata hivyo, ushawishi wake haukuhisika pakubwa katika safu ya mbele iliyotamalakiwa na Harvetz.

Pigo la pekee kwa Chelsea katika mchuano huo ni majeraha ambayo sasa yataweka nje Ziyech na kiungo Mateo Kovacic kwenye fainali ya Carabao Cup itakayokutanisha kikosi cha Tuchel na Liverpool ugani Wembley mnamo Februari 27, 2022.

“Ningemuondoa Mateo uwanjani katika kipindi cha kwanza. Hakim naye aliumia. Japo tuna siku kadhaa kabla ya fainali ya EFL Cup, nahisi kwamba hawatakuwa sehemu ya kikosi tutakachokitegemea wakati huo,” akasema Tuchel.

Kati ya wanasoka wa Chelsea waliotamba zaidi dhidi ya Lille ni Kante na beki mzoefu, Thiago Silva, 37. Vikosi hivyo vitarudiana mnamo Machi 16, 2022 nchini Ufaransa.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Mourinho apigwa marufuku na kutozwa faini kwa utovu wa...

ODM yalaumiwa vikali kuhusu fujo Mombasa

T L