• Nairobi
  • Last Updated May 13th, 2024 12:41 PM
Chipukizi Oduor afungia Barnsley goli ikizima Sheffield Wednesday

Chipukizi Oduor afungia Barnsley goli ikizima Sheffield Wednesday

Na GEOFFREY ANENE

BEKI Clarke Oduor alifunga goli safi Barnsley ikibwaga Sheffield Wednesday 2-0 katika mechi ya kujiandaa kwa msimu mpya wa 2021-2022.

Mzawa huyo wa Kaunti ya Siaya aliye na uraia wa Kenya na Uingereza, hakuwa ametumiwa na kocha Mfaransa Valerien Ismael kwa karibu michuano 30 ya mwisho ya msimu uliopita na kusemekana yuko mbioni kuhama klabu hiyo kutoka kaunti ya South Yorkshire.

Hata hivyo, kuwasili kwa raia wa Austria Markus Schopp kujaza nafasi ya Ismael aliyeelekea West Brom, kunaonekana kumempa Oduor mwamko mpya wa kupigania nafasi yake ugani Oakwell.

Schopp alianzisha Oduor katika kipindi cha pili ikishinda Rochdale 2-1 mnamo Julai 14 na kumpa dakika 30 za mwisho dhidi ya Sheffield Wednesday.

Hapo Julai 17, Jordan Williams alifungua ukurasa wa mabao dakika ya 22 kupitia kombora la nje ya kisanduku. Oduor aliongeza goli la pili dakika ya 70 alipochenga wachezaji wawili wa Wednesday na kisha kumpasiana mpira na Cameron Thompson kabla ya kukamilisha kwa ustadi.

Barnsley imepangiwa kuchuana na Watford hapo Julai 31 katika mchuano wake wa mwisho wa kujitayarisha kwa Ligi ya Daraja ya Pili ambayo wataanza dhidi ya Cardiff mnamo Agosti 7.

You can share this post!

Chelsea kuvunja benki ili kumsajili Robert Lewandowski...

Talaka ya Uhuru na Ruto baraka kwa Tanzania