• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Fidu aahidi makubwa kwa mashabiki wa Changamwe Ladies

Fidu aahidi makubwa kwa mashabiki wa Changamwe Ladies

NA ABDULRAHMAN SHERIFF

NAHODHA wa Changamwe Ladies FC, Fidu Namayi  amesema wanaahidi kufanya vizuri kwenye Ligi ya Soka la Wanawake ya jimbo la Pwani msimu huu wakiwa na nia ya kupanda ngazi hadi Ligi ya Taifa Daraja la Kwanza msimu ujao.

Fidu anasema yeye pamoja na wachezaji wenzake wamepania kuhakikisha wanashinda mechi zao za nyumbani na ugenini ili waweze kufanya vizuri, lengo lao kubwa likiwa ni kuibuka washindi wa ligi hiyo.

“Tunatambua ligi hii kuwa ni ngumu na timu zinazoshiriki ni kali, lakini tumepania kuhakikisha tunafanya vizuri ili msimu utakaofuata tuweze kupanda ngazi. Nia yetu kubwa zaidi ni kupanda hadi Ligi Kuu ya Soka la Wanawake,” akasema nahodha huyo.

Fidu anasema wameanza vizuri kwenye ligi hiyo kwa kuichapa Ocean D kwa mabao 2-0. “Ushindi huo wa mechi yetu ya kwanza unatupa matumaini makubwa ya kuhakikisha tunashinda mechi yetu ya pili dhidi ya Kilifi Ladies tutakayocheza ugenini,” akasema.

Fidu amesema wamefurahika mno kujiunga na ligi hiyo kwani wanashiriki wakifahamu kuna njia za kufika ligi kuu ikiwa watafanya vizuri katika ligi hiyo ya jimbo la Pwani. “Tunaamini tukipanda hadi ligi ya taifa, tutakuwa karibu kufika ligi kuu,” akasema.

Timu hiyo ya Changamwe Ladies ni miongoni mwa klabu maarufu za soka la wanawake ambayo imewahi kushiriki kwenye mashindano mbalimbali yakiwemo yale ya Coast Ladies Football Tournament yaliyofanyika huko Hola, Kaunti ya Tana River miaka miwili iliyopita.

  • Tags

You can share this post!

TAHARIRI: Lalama kuhusu CBC zisipuuzwe

DINI: Hakuna majira wala hali inayodumu milele, weka...