Na GEOFFREY ANENE
KAA Gent wameaibisha mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Ubelgiji Club Brugge kwa kuwamiminia magoli 6-1 ugani Ghelamco Arena, Jumapili.
Gent, ambao wameajiri beki Mkenya Joseph Okumu, walivuna ushindi huo mkubwa kupitia mabao ya Tarik Tissouadali dakika ya tisa, Julien De Sart dakika ya 15 (penalti), Nurio Fortuna (38), Roman Bezus (61), Laurent Depoitre (66) na kipa Mignolet aliyejifunga dakika ya 79. Brugge ilijifariji na bao kutoka kwa Hans Vanaken lililopatikana dakika ya 65.
Gent iliyonunua Okumu kutoka Elfsborg nchini Uswidi mwezi Juni kwa zaidi ya Sh440 milioni, inakamata nafasi ya tisa kwa alama saba baada ya kujibwaga uwanjani mara tano.
Brugge ni nambari tatu kwa alama 11 kutokana na mechi sita. Union Saint-Gilloise inaongoza kwa alama 12 ikifuatiwa na Eupen (11) kwenye ligi hiyo ya klabu 18.
Aidha, mabingwa wa Ubelgiji msimu 2014-2015 KAA Gent watamenyana na Partizan Belgrade, Flora Tallinn na Anorthosis Famagusta katika mechi za Kundi B za mashindano ya Ulaya ya daraja ya tatu maarufu kama Europa League Conference.
Gent ilikanyaga Rakow Czestochowa kutoka Poland 3-0 mnamo Agosti 27 na kujikatia tiketi ya kushiriki mechi za makundi za makala haya ya kwanza kabisa.
Buffalos, jinsi klabu ya Gent inavyofahamika kwa jina la utani, walitupa nje Czestochowa kwa jumla ya mabao 3-1 kupitia mabao ya Tarik Tissoudali, Vadis Odjidja-Ofoe na Julien de Sart.
Gent watakutana na wapinzani hao kutoka Estonia, Serbia na Cyprus kuanzia Septemba 16. Gent hutumia uwanja wa Ghelamco Arena unaobeba mashabiki 20,000.
Raundi ya 16-bora ni Machi 10-17, robo-fainali Aprili 7-14, nusu-fainali Aprili 28 nayo fainali itaandaliwa Mei 5 jijini Tirana nchini Albania.
Ratiba ya KAA Gent ya Europa Conference League:
Septemba 16 – Flora Tallinn vs KAA Gent (Estonia)
Septemba 30 – KAA Gent vs Anorthosis Famagusta (Ubelgiji)
Oktoba 21 – Partizan Belgrade vs KAA Gent (Serbia)
Novemba 11 – KAA Gent vs Partizan Belgrade (Ubelgiji)
Novemba 25 – Anorthosis Famagusta vs KAA Gent (Cyprus)
Desemba 9 – KAA Gent vs Flora Tallinn (Ubelgiji)
Makundi ya Europa League Conference 2021-2022:
Kundi A: LASK, Maccabi Tel-Aviv, Alashkert, HJK Helsinki
Kundi B: Gent, Partizan Belgrade, Flora Tallin, Anorthosis Famagusta
Kundi C: Roma, Zorya Luhansk, CSKA-Sofia, Bodo/Glimt
Kundi D: AZ Alkmaar, CFR Cluj, Jablonec, Randers
Kundi E: Slavia Praha, Feyenoord, Union Berlin, Maccabi Haifa
Kundi F: Copenhagen, PAOK, Slovan Bratislava, Lincoln Red Imps
Kundi G: Tottenham, Rennes, Vitesse, Mura
Kundi H: Basel, Qarabag, Kairat Almaty, Omonoia