• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 12:18 PM
Giroud akaribia rekodi ya mfungaji Thierry Henry nchini Ufaransa huku akiwa mchezaji mkongwe zaidi kuwahi kufungia miamba hao

Giroud akaribia rekodi ya mfungaji Thierry Henry nchini Ufaransa huku akiwa mchezaji mkongwe zaidi kuwahi kufungia miamba hao

Na MASHIRIKA

OLIVIER Giroud aliweka rekodi ya kuwa mchezaji mkongwe zaidi kuwahi kufunga bao katika historia ya timu ya taifa ya Ufaransa baada ya kuongoza mabingwa hao wa dunia kupepeta Austria 2-0 mnamo Alhamisi katika Uefa Nations League.

Ingawa Austria walianza mechi kwa matao ya juu, Ufaransa ndio walitangulia kubisha lango kupitia Kylian Mbappe na Aurelien Tchouameni. Bao la Mbappe halikuhesabiwa kwa kuwa alikuwa ameotea huku Tchouameni akishuhudia kombora lake likibusu mwamba wa goli la wageni wao.

Giroud alichangia bao la kwanza ambalo Ufaransa walifungiwa na Mbappe katika dakika ya 56. Giroud, 35, alipachika wavuni goli la pili la Ufaransa katika dakika ya 65.

Akiwa na umri wa mika 35 na siku 357, Giroud anamzidi Roger Marche aliyefungia Ufaransa dhidi ya Uhispania mnamo Disemba 1959 kwa siku 70.

Giroud kwa sasa anasalia na mabao mawili pekee ili kufikia rekodi ya Thierry Henry ambaye ni mfungaji bora wa muda wote wa Ufaransa kwa mabao 51.

Ufaransa ambao wangeteremshwa ngazi iwapo wangepigwa na Austria, walipaa juu ya Austria huku wakisubiri mchuano wa mwisho wa Kundi A1 dhidi ya Denmark mnamo Septemba 25, 2022.

Kundi hilo linaongozwa na Croatia waliokung’uta Denmark 2-1 jijini Zagreb.

Beki Borna Sosa aliyefunga bao la kwanza la kimataifa, aliwaweka Croatia kifua mbele kabla ya kiungo matata wa Manchester United, Christian Eriksen, kusawazisha mambo. Lovro Majer alifungia Croatia bao la ushindi.

Croatia sasa wana ulazima wa kushinda Austria mnamo Septemba 25, 2022 ili kufuzu kwa fainali za Nations League mnamo 2023 na kujikatia tiketi ya kunogesha mchujo wa kuingia fainali za Euro 2024.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Gharama ya kustarehe yapanda – CBK

Hasara lori la unga wa Sh2.6 milioni likipata ajali karibu...

T L