IMEKUSANYWA NA CECIL ODONGO
UWEZEKANO wa kiungo wa Manchester United Paul Pogba kuondoka timu hiyo unaendelea kuongezeka huku kandarasi yake ikitarajiwa itakamilika mwishoni mwa msimu huu.
Saini ya Pogba sasa inahemewa vikali na Real Madrid na iliyokuwa timu yake Juventus.
Mwanadimba huyo alizomewa sana na mashabiki wa Manchester United kwenye ushindi wa 3-2 walioupata dhidi ya Norwich wikendi iliyopita.
Hata hivyo, mashabiki hao walikashifiwa na Meneja wao Ralf Rangnick kutokana na tabia hiyo isiyopendeza akiwataka wasiwalenge wachezaji wake.
Pogba, raia wa Ufaransa, mwenyewe anadaiwa hayuko tayari kusalia United.
Alirejea Old Trafford mnamo 2016 akinunuliwa kwa kiasi kikubwa cha fedha kutoka Juventus na tangu wakati huo amesaidia the Red Devils kushinda League Cup pamoja na taji la Uropa.