• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 11:53 AM
Hatimaye dalili zaonekana za msimu mpya Ligi Kuu ya Kenya

Hatimaye dalili zaonekana za msimu mpya Ligi Kuu ya Kenya

NA RUTH AREGE

KOCHA wa timu ya Sofapaka ya Ligi Kuu ya Wanaume nchini (FKF-PL) David Ouma, anasema imekuwa vigumu kuandaa timu bila mwelekeo wa wazi kuhusu kuanza kwa msimu mpya na sasa wamepata afueni baada ya kutangazwa tarehe ya kuanza msimu huo.

Mnamo Jumatatu, Wakurugenzi Wakuu wa klabu za ligi kuu zilikutana kujadili tarehe ambayo ligi hiyo itaanza. Waliafikiana kuwa, ligi hiyo ya msimu wa 2022/23 itaanza kati ya tarehe 12 hadi 22 Novemba 2022.

Baada ya habari hiyo Ouma alisema, “Tumekuwa na wakati mgumu wa kuandaa wachezaji bila tarehe wazi ya kucheza. Jambo hili limekatisha tamaa wachezaji wengi. Kwa tarehe iliyowekwa, ni ahueni na sasa inatupa njia ya wazi ya kupanga timu.”

Kocha huyo wa ‘Batoto Ba Mungu’ aidha ameonyesha kuridhishwa na maandalizi ya timu hiyo wakati wanapojindaa kwa msimu mpya.

“Tumekuwa tukifanya mazoezi makali ya kujiandaa na msimu mpya na, kulingana na mechi ambazo tumecheza, nimefurahishwa na maandalizi yetu.”

“Kwa ujumla, nimeridhishwa na jinsi wachezaji wapya wanavyojituma mazoezini na katika mechi za kirafiki. Hili linadhihirika kutokana na matokeo ambayo tumekuwa tukiyasajili wakati wa mechi zetu za kirafiki. Kama makocha, ni wazi tuna wiki nne za kutumia vyema kabla ya msimu mpya,” aliongezea Ouma.

Suala la kupandishwa daraja na kushushwa daraja litakuwa mojawapo ya mambo ambayo Kamati Kuu ya Kitaifa ya FKF (NEC) italazimika kushughulikia.

Hata hivyo, klabu mbili ambazo zilipandishwa daraja, APS Bomet na Fortune Sacco FC hazikualikwa kwa mkutano huo.

Mathare United na Vihiga Bullets ambao walishuka daraja waliwakilishwa. Mbili hizo pia ziliwakilishwa katika mkutano wa awali ambapo klabu zilikubaliana kutoshiriki ligi inayoendeshwa na Kamati ya Mpito ya FKF. Waliahidi kucheza ligi inayoendeshwa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).

Mkurugenzi Mtendaji wa Nairobi City Stars Patrick Korir, alidumisha kwamba hawakujadili suala la kupandishwa daraja na kushushwa daraja wakati wa mkutano wa Jumatatu.

  • Tags

You can share this post!

Magnolia Girls Run kufanyika Novemba

Man-United wazamisha chombo cha Tottenham Hotspur katika EPL

T L