• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:50 AM
Jentrix Shikangwa na beki Ruth Ingotsi watarajiwa kujiunga na Simba Queens ya TZ

Jentrix Shikangwa na beki Ruth Ingotsi watarajiwa kujiunga na Simba Queens ya TZ

NA RUTH AREGE

WACHEZAJI wawili wa Harambee Starlets – mshambulizi Jentrix Shikangwa na beki Ruth Ingotsi Mukalukho – wanatarajiwa kujiunga na vinara wa Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania Simba Queens kwa mkataba wa mwaka mmoja.

Shikangwa atajiunga na Simba akitokea klabu ya Fatih Karagumruk S.K. inayoshiriki Ligi Kuu ya Uturuki. Hii ni baada ya mkataba wake wa muda mrefu na timu hiyo kukatika ghafla.

Kufikia mwisho wa Januari 2022, alihamia Uturuki kutoka Vihiga Queens ya KWPL, na kujiunga na Fatih Karagümrük iliyoanzishwa hivi karibuni kucheza Ligi Kuu ya Wanawake ya msimu wa 2021-22.

Mshambulizi Jentrix Shikangwa. PICHA | MAKTABA

Kwa upande mwingine, Ingotsi anatokea klabu ya Ligi Kuu ya Lacatamia yenye maskani yake Nicosia nchini Cyprus.

Alijiunga na klabu hiyo msimu wa 2020/21 akitokea Eldoret Falcons ya Ligi Kuu ya Wanawake nchini (KWPL).

Meneja wa klabu hiyo Selmana Makanya amethibitisha ujio wa wachezaji hao ambao anaamini wataisaidia Simba katika kuleta ushindani kwenye klabu msimu ujao.

“Ninaweza kuthibitisha kuwasili kwa Wakenya wengine wawili katika timu yangu kwa mkataba wa mwaka mmoja. Hatujaweza kuonana nao lakini tayari tumeshafikia makubalianao. Wakati wowote kuanzia leo tunawatarjia wawasili nchini Tanzania. Tunaimarisha kikosi chetu kabla ya msimu wa mpya wa 2022/23 ligi ya wanawake.” aliongezea Makanya.

“Tunajitayarisha pia kwa mashindano ya Kanda la Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), ambayo ni michuano ya Ligi ya Mabingwa ya Wanawake ya (CAF) nchini Morocco baadaye mwaka huu. Mashindano haya ni tofauti na ligi, lazima tuwe na kikosi kizuri ambacho kitatusaidia kutwaa ubingwa,” aliongezea Makanya.

  • Tags

You can share this post!

Uhispania watandikwa nyumbani kwa mara ya kwanza baada ya...

GASPO Women ya KWPL yasajili 10

T L