NA PATRICK KILAVUKA
KIOTA cha mashabiki wa Ingwe cha Kiambiu-Salem kimejengwa kwa msingi kwamba, ni timu ya soka ya mashabiki wa tawi la AFC Leopards almaarufu kama Ingwe.
Timu hii inapatikana Kiambiu-Jerusalem, japo inafanyia mazoezi yake katika uga wa Camp Toyoyo, Jericho.
Ina mashabiki 62 ambao wamo wanachezaji 24, chini ya benchi ya kocha Evans Mbiti, naibu wa kocha Musa Jumba, timu meneja Reagan Buluku, nahodha Bonface Shikuri, kinara Erick Onzere na mwenyekiti wa mashabiki Caroline Saga.
Madhumuni ya kuasisi jamii hii inayoinua soka kwa hali na mali ilikuwa kuhakikisha kwamba, kuna msingi imara wa mashabiki wa timu ya Ingwe eneo la Eastleigh Kusini na Jericho kupeperusha bendera yake ya uwakilishi mashinani ukikumbatia matabaka mbalimbali ambao ni wafuasi wa Ingwe.
Pili, ilinuiwa kuwa mmojawapo ya matawi ya kufanikisha sapoti ya mashinani.
Kuisaidia kukuza vipaji ambavyo vinainua timu kubwa.
Isitoshe, kusaidia timu hii na klabu kuu ya Leopards kwa hali na mali.
Timu hii ya ufuasi kwa Ingwe, huchangia sapoti na uhisani wao kwa klabu hiyo kwani, kila shabiki hutoa ada ya usajili wa Sh1,500 ambapo kulingana na wadau kiasi fulani huenda kwa klabu na kiasi kingine hubakia kama salio la kushughulikia mikakati ya tawi hili.
Wao huhudhuria michuano ya AFC Leopards.
Timu hii ina matarajio ya kujisajili kwenye ligi ya FKF baada ya msimu ujao kwani wana imani kwamba, timu itakuwa na uwezo wa kujihimili kwa mujibu wa matakwa ya ligi hiyo.
Hata hivyo, wanaendeleza kampeni yao ya kukuza vipawa ambavyo vinaweza kusajiliwa na klabu kuu ikiwa wamechomoa kiungo Dan Alex ambaye amesajiliwa na AFC Leopards Youth.
Kiambiu Salem ilicheza mchuano wa kujipima nguvu dhidi ya Real Stars na kuambulia sare ya 1-1 ugani Kihumbuini.
Mshikamano wa timu umekumbatia wanachama wa klabu ambao hawana mipaka ya ukabila na wanasaidiana.
Pia, wana ushirika ambapo endapo wao hufaana kwa faraja na dhiki kama jamii.
Pia, wanahimiza udumishaji wa nidhamu kama nguzo ya maadili mema ya jamii kwa mashabiki kupitia kushauriana.
Wanatarajia kuwa wanafanya uchaguzi wao wa tawi baada ya miaka minne.
Changamoto za fedha bado zingalipo, japo wamejifunga kibwebwe kuhakikisha jahazi la tawi na timu halitumbukii.
Mipango yao ni kujaribu kutia motisha mashabiki chipukizi kujisajili ili mashinani kuwa na msingi imara wa kujenga timu kuu ya Ingwe mbali na kuhimiza uwepo wa matawi mengine mashinani.