• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Kombe la Dunia lilikuwa na ufanisi mkubwa

Kombe la Dunia lilikuwa na ufanisi mkubwa

NA JOHN ASHIHUNDU

KWA muda wa mwezi mmoja, mashabiki wa soka kote duniani walitosheka na burudani ya michuano ya Kombe la Dunia iliyomalizika kwa kishindo nchini Qatar, Jumapili.

Ufanisi wa uaandalizi wa fainali hizo umemfanya Rais wa Shirikisho la Kimataifa la Soka (Fifa) Gianni Infantino kutaja mashindano hayo kama yaliyofana zaidi tangu yafanyike kwa mara ya kwanza nchini Uruguay, miaka 92 iliyopita.

Kulingana na Infantino, ufanisi huo umeondoa dhana kwamba mataifa madogo kama Qatar hayana uwezo wa kuandaa mashindano makubwa ya kimataifa.

Mashindano hayo ya Makala ya 22 yalileta pamoja timu 32 zilizoshindana tangu Novemba 20, ambapo Argentina iliibuka na ushindi dhidi ya Ufaransa waliokuwa mabingwa watetezi.

Ni fainali ambayo itakumbukwa milele, kutokana na sababu kwamba timu hizo zilicheza kwa dakika 120, mabao yakiwa 3-3 na ilibidi mwamuzi wa mechi aagize mikwaju ya penaltii kupigwa kutafuta mshindi.

Ufanisi mwingine ni kwa timu zilizowakilisha bara Afrika- Morocco, Senegal, Cameroon, Tunisia na Ghana ambazo angalau kila moja iliandikisha ushindi.

Timu iliyovuma zaidi katika wawakilishia hao wa Afrika ni Morocco ambayo pamoja na kuibwaga Uhispania kupitia kwa mikwaju ya matuta (3-0), katika raundi ya 16-Bora kabla ya kuibwaga Ureno kwenye robo-fainali kwa 1-0 na kufuzu kwa nusu-fainali.

Baada ya kuweka historia hiyo kama nchi ya kwanza kutinga hatau ya nusu-fainali katika mashindano hayo, vijana hao wa kocha Walid Regragui walibanduliwa 2-0 na Ufaransa, na kumaliza katika nafasi ya nne baada ya kushindwa na Croatia kwa 2-1.

Kabla ya kuweka rekodi hiyo, ni mataifa matatu tu- Cameroon, Senegal na Ghana ambazo zilifika hatua ya robo-fainali, Cameroon ikianza mnamo 1990 nchini Italia, Senegal zilipofanyika kwa pamoja nchini Japan na Korea Kusini na baadaye Ghana nchini Afrika Kusini.

Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa michuano hiyo kufanyika katika eneo la Mashariki ya Kati na ardhi ya Uarabuni kwa mara ya kwanza.

“Fifa kwa jumla imepongeza fainali za Kombe la Dunia za mwaka huu, pamoja na watu wote waliohusika kuzifanikisha,” Infantino alisema katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika Doha kabla ya fainali kufanyika Jumapili.

Kiongozi huyo wa Fifa alisema kadhalika baraza hilo limekubali kuidhinisha baadhi ya mapendekezo, ikiwa pamoja na kupandisha bajeti ya fainali zijazo zitakazofanyika baada ya miaka mine.

Infantino alisema bajeti ya msimu wa 2023-2026 itagharamiwa kwa bajeti ya Sh923 bilioni, kutoka kwa 787 bilioni zilizotumika msimu wa 2018-2022.

Fifa kawaida hutoa msaada wa kifedha kwa mashirika wanachama wake. Kwa mfano Kenya ilipokea ufadhili wa Sh120 milioni, kulingana na taarifa ya matumizi ya kifedha iliyotolewa na shirikisho hilo la kimataifa.

“Tayari baraza la Fifa limepitisha bajeti ya Sh1.35 bilioni kutumika kwa miaka mine ijayo, ambapo Sh246 bilioni zitatumika kuimarisha vipaji chini ya aliyekuwa kocha wa Arsenal, Arsene Wenger, ambaye ni Mkuu wa Kimataifa wa kuimarisha vipaji katika kitengo cha shirikisho hilo.

Fifa ilieleza mpango huo wa 2023-2026 kuwa mkubwa zaidi kuwahi kufanyika, ambao madhumuni yake ni kusaidia mashirika yake kufikia upeo wa juu kimataifa.

Alisema, mashindano ya wanasoka wasiozidi umri wa miaka 17 kwa timu za wavulana na wasichana yatafanyika kila mwaka, ambapo idadi ya timu zitakazoshirki itaongezeka kutoka 24 kwa timu za wavulana na 16 za wasichana. Mechi za Kombe la Klabu Bingwa zitafanyika nchini Morocco mwezi Februari 2023.

Infantino alisema nchini Qatar, mechi moja imekuwa ikivutia mashabiki 52,760, wakati idadi ya juu zaidi ikifikia 88,666 wakati wa mechi ya Kundi C kati ya Argentina na Mexco iliyochezewa Lusail Stadium. Kufikia sasa, mashabiki wapatao 3.7 milioni wamehudhuria mechi 62 zilizochezwa.

  • Tags

You can share this post!

Hatimaye ndoto ya Messi yatimia

Qatar yaweka rekodi kwa kuandaa Kombe la Dunia katika...

T L