• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 10:50 AM
KPA waridhika nambari sita Afrika mpira wa vikapu

KPA waridhika nambari sita Afrika mpira wa vikapu

Na GEOFFREY ANENE

MALKIA wa mpira wa vikapu nchini Halmashauri ya Bandari za Kenya (KPA) wamekamilisha mashindano ya klabu za Afrika katika nafasi ya sita mjini Maputo, Msumbiji, Jumamosi.

Vipusa wa kocha Anthony Ojukwu wamepoteza 71-51 dhidi ya ASC Ville de Dakar kutoka Senegal katika mechi ya kuorodhesha nambari tano na sita.

KPA ilishinda robo ya kwanza 14-12 kupitia kwa pointi za Madina Okot (sita), Natalie Akinyi (tatu), Selina Okumu (mbili) na Brenda Wasuda (tatu). Ifunaya Okoro kutoka Nigeria aliimarisha uongozi wa KPA hadi 16-12 mapema katika robo ya pili, lakini Couna Ndao alifungia Dakar pointi tatu na kupunguza mwanya huo hadi 16-15. Pointi mbili kutoka kwa Fatoumata Traore ziliweka Dakar 17-16 juu zikisalia dakika 7 na sekunde 27 kufika kipindi cha mapumziko. Kutoka hapo, KPA ilijaribu bila mafanikio kuziba mwanya ulioendelea kuongezeka hadi 13 baada ya kupoteza robo ya pili 24-9. Mabingwa hao wa zamani wa Zoni ya Tano ya Afrika walinyakua robo ya tatu 14-12, lakini wakapoteza tena mwelekeo katika robo ya mwisho wakisalimu amri 23-14. Okot alifungia KPA pointi nyingi (16) naye Ndoumbe Mbodj akawa mfungaji bora wa Dakar (15).

Mchuano huo ulitanguliwa na ule wa kutafuta nambari saba na nane ambao C.N.S.S. kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ilipepeta APR kutoka Rwanda 72-52.

Nambari tatu na nne itakuwa kati ya mabingwa watetezi Inter Clube kutoka Angola na Ferroviario Maputo (Msumbiji). Fainali itakutanisha Costa do Sol (Msumbiji) na Sporting Alexandria (Misri). Energie BBC ilimaliza nambari tisa (mwisho).

  • Tags

You can share this post!

DARUBINI YA WIKI: Toleo Nambari 16 | Desemba 18, 2022

KOMBE LA DUNIA FIFA 2022: Argentina yaizidi maarifa...

T L