Na JOHN KIMWERE
KOCHA wa timu ya wanaume ya Chuo Kikuu cha Kenyatta (KU), Victor Luvale anakiri kuwa wanatarajia mtihani mgumu kwenye shindano la Super Cup.
Hata hivyo anashilikia kuwa wamepania kujituma kwa udi na uvumba wakilenga asema wamepania kutinga nusu fainali kwenye kidumbwedumbwe hicho. KU itashiriki kipute hicho baada ya kuibuka ya sita katika jedwali ya Ligi Kuu msimu uliyopita.
”Tumepania kupambana kiume kwenye mechi hizo tukaocheza na miamba wa handiboli nchini ikiwamo Black Mamba na Halmashauri ya Nafaka na Mazao nchini (NCPB),” alisema na kuongeza kamwe hawana hofu bali wanaamini wanaweza.
Itakuwa mara ya pili KU kushiriki kipute hicho tangia mwaka 2014. Kocha huyo anadokeza kuwa wanaendelea na maandalizi kujiweka tayari kwa kipute hicho. Katika ratiba ya michuano hiyo KU imepangwa Kundi B linalojumuisha Kenya General Service Unit (GSU) na Chuo cha Strathmore.
Nalo Kundi A linashikisha Jeshi la Ulinzi (KDF), Black Mamba na NCPB. KU itafungua kampeni zake dhidi ya Strathmore kisha itakutanishwa na GSU.
KU inajivunia wachezaji kadhaa akiwamo Samuel Katuva (nahodha), naibu wake Morgan Simiyu, Dickson Wanyama, Fresnel Khisa, Amos Keter na Isaac Nyongesa.