• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Lewandowski afunga mabao mawili na kuongoza Bayern kuwaponda Dynamo Kyiv kwenye UEFA

Lewandowski afunga mabao mawili na kuongoza Bayern kuwaponda Dynamo Kyiv kwenye UEFA

Na MASHIRIKA

ROBERT Lewandowski alifunga mabao mawili na kusaidia waajiri wake Bayern Munich kupepeta Dynamo Kyiv ya Ukraine 5-0 katika mchuano wa Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Jumatano usiku uwanjani Allianz Arena, Ujerumani.

Ushindi huo ulikuwa wa pili kwa Bayern kusajili baada ya kufungua kampeni zao za Kundi E kwa kupokeza Barcelona ya Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) kichapo cha 3-0 mnamo Septemba 14, 2021.

Lewandowski alifunga katika mchuano wake wa sita mfululizo wa UEFA alipowafungulia Bayern ukurasa wa mabao kupitia penalti ya dakika ya 12.

Alipachika wavuni goli la pili kunako dakika ya 27 baada ya kukamilisha krosi ya Thomas Muller ambaye pia alimtatiza pakubwa kipa wa Dynamo Kyiv, Georgiy Bushchan.

Mabao mengine ya Bayern yalifumwa wavuni kupitia Serge Gnabry, Leroy Sane na Eric Maxim Choupo-Moting. Bayern ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga), walinyanyua taji la UEFA mnamo 2019-20 baada ya kuzamisha chombo cha Paris Saint-Germain (PSG) kwenye fainali iliyochezewa jijini Lisbon, Ureno.

Kufikia sasa, wamefunga mabao manane kutokana na mechi mbili za ufunguzi wa Kundi E linalojumuisha pia Barcelona, Dymano Kyiv na Benfica ambao watavaana nao katika mchuano ujao wa UEFA.

  • Tags

You can share this post!

Google kufuta jumbe potovu kuhusu chanjo ya corona YouTube

Juventus wazamisha chombo cha Chelsea ambao ni mabingwa...