• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Mamelodi Sundowns, Kaizer Chiefs zaingia Klabu Bingwa makundi

Mamelodi Sundowns, Kaizer Chiefs zaingia Klabu Bingwa makundi

Na GEOFFREY ANENE

KLABU ya Mamelodi Sundowns anayochezea beki Brian Mandela Onyango na Kaizer Chiefs inayoajiri kiungo Anthony Agay Akumu zimetinga mechi za makundi za Klabu Bingwa Afrika, Jumanne.

Sundowns imechabanga Jwaneng Galaxy kutoka Botswana kwa jumla ya mabao 5-1 baada ya kushinda mechi ya marudiano ya raundi ya kwanza 2-0 uwanjani Loftus Versfeld nchini Afrika Kusini.

Mothobi Mvala na mshambuliaji Mnamibia Peter Shalulile walifunga katika mechi ya mkondo wa kwanza mjini Lobaste mnamo Desemba 22, 2020.

Mshambuliaji Kermit Erasmus, Mvala na beki Thapelo Morena walitikisa nyavu za Jwaneng katika mechi ya marudiano iliyotamatika 3-1.

Waliona lango dakika ya 39, 68 na 81 mtawalia kabla ya Jwaneng kupata la kufutia machozi dakika ya 89 kupitia kwa Tebogo Sembowa.

Onyango, ambaye alifungia Sundowns almaarufu ‘the Brazilians’ bao lililozamisha Orlando Pirates kwenye Ligi Kuu ya Afrika Kusini (PSL) Januari 2, alipata nafasi mbili nzuri dhidi ya Jwaneng hapo Jumanne, moja ikizalisha kona. Pia, alizuia kombora moja hatari kutoka kwa Ricardo Lourenco mapema katika mchuano huo.

Chiefs, ambayo ilikabwa 0-0 katika mechi ya mkondo wa kwanza Desemba 23 mwaka jana mjini Johanesburg, ilizamisha wapinzani wao Primeiro de Agosto 1-0 nchini Angola mjini Luanda.

Ilipata bao hilo muhimu kupitia kwa mshambuliaji wa Zimbabwe Khama Billiat dakika ya 41.

Chiefs haikusafiri na Akumu katika mechi hiyo iliyosakatiwa uwanjani 11 de Novembro.

Jumatano itakuwa zamu ya Simba SC ambayo imeajiri Wakenya Joash Onyango na Francis Kahata kukaribisha FC Platinum nchini Tanzania. Platinum ilishinda mechi ya mkondo wa kwanza 1-0 nchini mwake Zimbabwe mnamo Desemba 23.

Mabingwa wa Kenya, Gor Mahia pia watakuwa uwanjani Nyayo hapo Jumatano wakihitajio muujiza wa mabao 7-0 dhidi ya CR Belouizdad kusonga mbele.

Belouizdad iliaibisha Gor 6-0 nchini Algeria katika mchuano wa mkondo wa kwanza Desemba 26.

You can share this post!

Jubilee na ODM njia panda kuhusu uchaguzi mdogo wa ugavana...

Umeme Bees na mabingwa watetezi Kingstone FC wadenguliwa...