• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 7:50 AM
Modern Coast kuingia vitani kuhakiklisha inabakia kwenye NSL

Modern Coast kuingia vitani kuhakiklisha inabakia kwenye NSL

Na ABDULRAHMAN SHERIFF

KOCHA wa Modern Coast Rangers FC, Mohamed Ahmed almaarufu Mohaa ametangaza timu yake kuwa katika vita vikali vya kimchezo watakavyopigana kuhakikisha wanajinasua kutoka nafasi ya hatari ya kuteremshwa ngazi.

Mohaa alikuwa akiongea na kuwapongeza wachezaji wake kwa kucheza kwa moyo wao wote na kupigana vita vya kimchezo kuhakikisha wamepata ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Silibwet FC kutoka Bomet. Anasema vita hivyo vinaendelea hadi mwisho wa ligi hiyo.

Anasema wanasoka wake walicheza kwa kujitolea mhanga na soka la hali ya juu na kustahili kupata ushindi huo mkubwa ambao anaamini utawapa motisha wa kucheza vizuri zaidi kwenye mechi zao zilizobakia.

“Kwa hakika tuko katika nafasi mbaya katika ligi hii lakini jinsi wachezaji wangu walivyocheza kama wako vitani, sio vita vya kawaida bali vya kimchezo, kuhakikisha wanaibuka washindi, kumenifurahisha na nina tamaa kubwa tutaepuka nafasi za chini,” akasema.

Alisema kwa muda wote wa mchezo, tangu uanze hadi firimbi ya mwisho, wachezaji wake walionyesha kuwa na hasira na kiu cha kufunga mabao na hilo ndilo liloisaidia timu yake hiyo kupata ushindi na akaeleza matumaini ya kupata ushindi kwenye mechi zao zote zilizobakia.

Kocha wa Silibwet FC, Patrick Amuoka alisema huenda sababu kubwa iliyowafanya kupoteza mechi hiyo kwa mabao mengi ni kutokana na uchovu wa safari ndefu ya usiku kucha.

“Sababu ya safari ndefu bila ya kupumzika imewafanya wanasoka wangu wasicheze kandanda ya kawaida,” akasema.

Katika mechi hiyo, Innocent Kiprotich wa Modern Coast alifunga mabao mawili katika dakika za 17 na 85 hali Jamal Mwanyoa na Bakari Juma wakatinga nyavu dakika za 30 na 58 mtawalia.

You can share this post!

Msako kuzima tabia ya uunganishaji stima kinyume cha sheria

Radi yaua 60 wakiwemo 11 waliokuwa wakipiga ‘selfie’