NA GEOFFREY ANENE
MIGUEL Almiron amejitokeza kwa nguvu kwenye Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu wa 2022-2023 akichezea Newcastle United.
Kiungo huyo mshambulizi amecheka na nyavu mara tisa na kusuka pasi moja ya mwisho iliyoishia kuwa bao.
Mapema juma hili, Almiron alitetemesha nyavu za Leicester mara moja wakati Newcastle ilitamba 3-0 katika mechi ya raundi ya 16.
Ni msimu wake mzuri tangu ajiunge na Newcastle msimu 2018-2019. Alichangia mabao manne msimu 2019-2020 na tena idadi hiyo 2020-2021 na kuona lango mara moja 2021-2022.
Grafu yake imeimarika msimu huu ambapo Newcastle inaonesha dalili ya kusumbua katika vita vya kuwania nafasi ya kushiriki Klabu Bingwa Ulaya.
Almiron alianzia soka yake katika timu ya Club 3 de Noviembre nchini Paraguay akiwa na umri wa miaka saba.
Alipitia pia mikononi mwa Cerro Porteno akipata nafasi zaidi za kuonyesha talanta yake katika timu ya wachezaji wasiozidi umri wa miaka 17.
Almiron alipiga hatua nzuri katika uchezaji wake alipojiunga na Club Atletico Lanus nchini Argentina mwezi Agosti 2015.
Alijitokeza kuwa muhimu katika kikosi cha Lanus mwaka 2016 wakishinda Ligi, ikiwemo kufunga mabao dhidi ya majirani Banfield katika gozi la Clasico del Sur, na baadaye dhidi ya San Lorenzo.
Alichangia pasi iyozalisha bao la pekee dhidi ya Racing wakati Lanus ilibeba taji la Copa Bicentenario.
Almiron aliondoka Lanus hapo Desemba 5, 2016 na kujiunga na Atlanta United iliyokuwa imejumuishwa katika Ligi Kuu ya Amerika na Canada (MLS) kwa mara ya kwanza kabisa.
Alijizolea umaarufu kambini mwa Atlanta United FC.
Katika msimu wa kawaida, Almiron alijumuishwa mara saba katika timu ya wiki ya MLS, na mara mbili kama mchezaji bora wa juma.
Mwisho wa msimu huo, Almiron alitajwa katika timu ya wachezaji 11 bora na mshindi wa tuzo ya mchezaji mgeni wa mwaka.
Mnamo Aprili 2018, Almiron aliibuka mchezaji bora wa mwezi wa MLS baada ya kutetemesha nyavu mara tano na kumega pasi mbili zilizojaa wavuni huku Atlanta ikiandikisha ushindi mara tatu na sare moja mwezi huo.
Msimu ulikamilika akiwa na mabao 12 na pasi 14 za mwisho zilizoishia kuwa magoli na kujumuishwa katika kikosi cha wachezaji 11 bora wa MLS.
Atlanta ilinyakua taji la Kombe la MLS 2018 dhidi ya Portland Timbers.
Almiron aliyoyomea Newcastle United.
Hasikitishi kila anapoingia uwanjani. Anafahamika kwa kasi, chenga na makombora.
Kimataifa, Almiron hupeperusha bendera ya Paraguay.
Subscribe our newsletter to stay updated